Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein ameondoka nchini leo kwenda nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) kwa ziara ya wiki moja kufuatia muwaliko wa viongozi wa nchi za Umoja huo.Ziara hiyo ya Dk. Shein inatarajiwa kuanza kesho tarehe 21 na kumaliza tarehe 27 Januari mwaka huu katika nchi hizo za (UAE), ambapo ataanza ziara yake kwa kufanya mazungumzo na Mtukufu Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan, Mrithi wa Mtawala wa Abu Dhabi na Naibu Amiri Jeshi Mkuu wa Vikosi vya Ulinzi vya (UAE) nchini Abu Dhabi.

Akiwa mjini Abu Dhabi Dk. Shein atakutana na Mhe. Mohamed Saif Suwaid, Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo ya Abudhabi “Abudhabi Fund for Development”, atatembelea mji wa Nishati, Masdar, atatembelea jumba la kumbukumbula Louvre, msikiti wa Shaikh Zayed pamoja na sehemu ya kihistoria ya Wahat Al Karama.Aidha,Dk. Shein afanya ziara Dubai na kukutana na kufanya mazungumzo na Mtukufu Shaikh Mohammed bin Rashid Al Makhtoum, Makamo wa Rais na Waziri Mkuu wa (UAE) na Mtawala wa Dubai.

Rais Dk. Shein akiwa Dubai atatembelea Maeneo Huru na Bandari ya Jebel Ali, atakutana na Jumuiya ya Wafanyabiashara, wawekezaji na wenyeviwanda wa Dubai na kutembelea Mji mpya wa kisasa wa Nakheel pamoja na Mradi wa Palm Jumeirah.Katika nchi hizo za Umoja wa Falme za Kiarabu, Pia, Dk. Shein atafanya ziara mjini Sharjah na kukutana pamoja na kufanya mazungumzo na Mtukufu Dk. Shaikh Sultan Mohammed Al Qasimi, Mtawala wa Sharjah.

Akiwa Sharjah, Dk. Shein atatembelea katika eneo la shughuli za uvuvi la ‘East Fishing Processing LLC”, atatembelea shamba la ngombe wa maziwa la Al Rawabi, pamoja na kutembelea mji wa michezo wa Dubai.Sambamba na hayo, Dk. Shein pia, atafanya ziara Ras Al Khaimah na kukutana pamoja na kufanya mazungumzo na Mtukufu Shaikh Saud Saqr Al Qasimi, Mtawala wa Ras Al Khaimah pamoja na kutembelea eneo la Kampuni ya Kimataifa ya Utafiti na Uchimbaji wa Mafuta na gesi asilia ya Ras Al Khaimah “Rak Gas”
.
Katika ziara hiyo, Dk. Shein amefuatana na viongozi mbali mbali akiwemo Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein, Waziri wa Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Salama Aboud Talib, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Khalid Salum Mohamed, Waziri Asiyekuwa na Wizara Maalum Juma Ali Khatib,pamoja na Mshauri wa Rais Masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Uchumi na Uwekezaji Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa.

Wengine ni Katibu Mkuu Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko, Juma Ali Juma, Balozi Mohamed Haji Hamza Kaimu Mkurugenzi Idara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa upande wa Zanzibar pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Uwekezaji Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA) Salum Khamis Nassor na watendaji wengine wa Serikali.
 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein anatarajiwa kurejea nchini Jumamosi, tarehe 27 Januari, 2018.Katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume Dk. Shein aliagwa na viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa na Serikali, viongozi wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama pamoja na wananchi ambao waliongozwa na Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd.