Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi alikuwa mgeni rasmi katika Burudani ya muziki wa Taarabu asilia, ilioandaliwa maalum kwa ajili ya maadhimisho ya kusherehekea miaka 58 ya Mapinduzi ya Zanzibar.Hafla hiyo imefanyika katika Ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdul-wakil, Kikwajuni jijini Zanzibar, ambapo magwiji wa sanaa ya muziki wa Taarabu asilia kutoka Kikundi cha Taifa Zanzibar, walionyesha umahiri wao katika kuchararaza nyuzi na kughani nyimbo mbali mbali na kukonga nyoyo za mashabiki wa sanaa hiyo kutoka Mikoa yote ya Zanzibar.

Katika burudani hiyo nyimbo mbali mbali zilizopata kuvuma na kupendwa kutoka kwa watunzi wabobezi na waimbaji nguli wa sana hiyo zilipata fursa ya kuimbwa na kuibua vifijo na nderemo.

Nyimbo ya kwanza ambayo ilifungua pazia la burudani hiyo, ilikuwa ni ile ilioendana na maudhui ya sherehe hizo, ambapo Mwimbaji nguli Al-anisa Fatma Dawa alighani kwa ustadi mkubwa na kuwafanya watazamaji kuinuka kwenye viti na kumtunza.Aidha, kumalizika kwa nyimbo hiyo, kulitoa fursa kwa mwimbaji mahiri Al - anisa Hilda Mohamed kughani nyimbo maarufu na iliowahi kupata sifa kubwa hapa Zanzibar, ijuilikanayo kwa jina la ‘Nisubiri hadi lini’.

Kadri muda ulivyosonga, ndivyo Burudani hiyo ya taarabu iliendelea kunoga na kuufanya usiku huo kuwa maalum kwa wapenzi na mashabiki wa sanaa hiyo, hususan pale zilipoimbwa nyimbo maarufu kama vile, Cheo chako, Kibali, Kweli ninae, Mpewa hapokonyeki, Lulu, Ubinafsi na choyo, Lipi nilopenda kwako na kuhitimishwa na nyimbo ya Wahoi.

Nyimbo nyengine zenye mnasaba na maudhui ya sherehe hizo ambazo zilipata nafasi ya kuimbwa na kuibua shwangwe kubwa, ni pamoja na ile ya kumpongerza Dk. Mwinyi kwa Uongozi wake, ilioimbwa na msanii nguli Nassor Hussein.Katika hafla hiyo, ambapo Rais Dk. Mwinyi aliambatana na Mama Mariam Mwinyi,  watazamaji na mashabiki wa sanaa ya taarabu asilia walikoshwa na kupata kile mioyo yao inapenda, baada ya kuwashuhudia wasanii nguli kama vile Ustadh Idd Sued (mpendwa na wengi) na Profesa Mohamed Elias wakiendelea kuimba kwa sauti ile ile iliyozoeleka kwa miaka na dahari na kuthibitisha ule usemi wa ‘vya kale ni dhahabu’.

Viongozi mbali mbali wa Kitaifa, akiwemo Makamo wa Pili wa Rais Hemed Suleiman Abdalla walishiriki.