RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ameeleza utayari wa Serikali ya Awamu ya Nane katika kushirikiana na Benki ya NMB kwa ajili ya kuimarisha uchumi pamoja na huduma za kijamii Zanzibar.Hayo ameyasema leo wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na uongozi wa Benki ya NMB Ikulu Jijini Zanzibar ukiongozwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki hiyo Bi Ruth Zaipuna .

Katika maelezo yake Rais Dk. Hussein alisema kuwa Benki ya NMB imepata mafanikio makubwa hivyo, Serikali anayoiongoza iko tayari kushirikiana na Benki hiyo katika kuimarisha miradi mbali mbali ya kiuchumi sambamba na huduma za kijamii.Alisema kuwa katika kuendeleza na kuimarisha miradi ya maendeleo ikiwemo afya na elimu Serikali anayoiongoza iko tayari kutoa ushirikiano wake kwa Benki hiyo ili iweze kuunga mkono juhudi za Serikali katika sekta hizo ambazo wamekuwa wakitoa misaada yao.Rais Dk. Hussein alisema kuwa Serikali iko tayari kukopa fedha kwa ajili ya kuwatafutia maeneo wajasiriamali ili iweze kuwasaidia katika kufanya shughuli zao.

Alisema kuwa upo umuhimu kwa Benki hiyo katika kuwakopesha wajasiriamali wadogo wadogo ikiwa ni pamoja na kuwasaidia katika kuwapa mitaji, kuwawekea mazingira mazuri ya kufanyia shughuli zao sambamba na kuwapa mafunzo ili waweze kufanya shughuli zao kwa ufanisi mzuri zaidi.Aidha, Rais Dk. Hussein alieleza kuwa Serikali inahitaji mashirikiano katika eneo la elimu na afya ambapo kwa upande wa sekta ya Elimu bado msaada wa madawati unahitajika hasa ikizingatiwa kwamba vijana wanaoandikishwa skuli ni wengi.

Hata hivyo, Rais Dk. Hussein alisisitiza haja katika kuiunga mkono Sekta ya Afya, bado kuna mahitaji mbali mbali yakiwemo vifaa tiba, rasilimali watu na vyenginevyo.Pamoja na hayo, Rais Dk. Hussein aliuhakikishia uongozi huo wa Benki ya NMB kwamba Serikali itaendeleza ushirikiano wake na iwapo kutatokea urasimu na vikwazo vyovyote itakavyofanyiwa Benki hiyo basi wasisite kutoa taarifa.

Alieleza umuhimu wa kuwepo kwa mifumo madhubuti ya kukushanya kodi ambapo alieleza utayari wa Serikali kutumia wataalamu wake kushirikiana na Benki hiyo ya NMB katika kuhakikisha huduma hiyo inafanikiwa na nchi kuweza kunufaika kiuchumi.

Rais Dk. Hussein alieleza haja ya kwa upande wa miradi mikubwa kuwepo kwa mipango madhubuti ya utekelezaji wake ambapo Benki hiyo pia, inahitajika kutoa ushirikiano wake.Aliongeza kuwa ni masharti ya Benki hiyo ni vyema yakaendana na uwezo wa Serikali na kuangalia mi miradi gani benki hiyo ingeweza kushirikiana na Serikali kwa mashirikiano ya pamoja na wataalamu waliopo.

Mapema Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki hiyo ya NMB, Bi Ruth Zaipuna   alimpongeza Rais Dk. Hussein Mwinyi kwa ushindi wa kishindo alioupata huku akiahidi kwamba Benki ya NMB itaendelea kumuunga mkono yeye na Serikali yake katika kuhakikisha uchumi wa Zanzibar unaimarika.

Alisema kuwa benki hiyo iko tayari kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Nane katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo zikiwemo zile za kiuchumi na kijamii.

Akitoa historia ya Benki hiyo, Bi Ruth Zaipuna alisema kuwa Benki hiyo ilianzishwa kwa Sheria ya Bunge ya ‘National Microfinance Bank’ ya mwaka 1997 baada ya kuvunjwa iliyokuwa Benki ya Taifa ya Biashara kwa mujibu wa Sheria ya Bunge.

Alisema kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilibinafsisha Benki ya NMB kwa kuuza asilimia 49 ya hisa zake kwa Ushirika uliokuwa ukiongozwa na Rabo Bank huku akieleza kwamba Benki hiyo ina uwezo wa kukopesha mteja mmoja hadi kiasi cha TZS Bilioni 230.Aliongeza kuwa benki hiyo ya biashara iko imara katika kutekeleza kazi zake ikiwa ni pamoja na kusaidiana na Serikali ya Awamu ya Nane kwani imejiandaa vyema na ina mtaji wa kutosha unaofika Tirioni 7.
Alisema kuwa Benki hiyo iko tayari kushirikiana na Serikali kama mdau mkuu wa kifedha katika kuongeza kasi ya utekelezaji wa dira ya Rais Dk. Hussein mwinyi ya kuimarisha uchumi wa Zanzibar.

Aidha, kiongozi huyo wa NMB alisema kuwa Benki hiyo iko tayari kushirikiana na Serikali katika kuwezesha miradi ya kimkakati ya Serikali.Pamoja na hayo, alieleza kuwa Benki hiyo ipo tayari kutumia uwezo na uzoefu wake mkubwa wa kiteknolojia pamoja na ubunifu katika kutoa suluhisho la huduma za kielektroniki kwa Serikali.

Bi Zaipuna alieleza uzoefu wa Benki hiyo katika ukusanyaji wa kodi kidigitali ambapo tayari imeshafanya shughuli hizo kwa taasisi mbali mbali ikwemo TANAPA, NCAA, Hospitali, Huduma za malipo kwa taasisi za Serikali, TASAF,TRA na nyenginezo.Alieleza kuwa kwa gawio la Serikali ya Jamhuri ya Mungano wa Tanzania kwa mwaka 2019 lilikuwa ni TZS Bilioni 15.3.

Mtendaji Mkuu huyo wa NMB alisema kuwa Benki yake ameweza kuchangia katika sekta ya elimu kwa kutoa madawati yapatayo 45,000 kwa skuli za msingi na sekondari, kompyuta 1,270, vituo vya afya 460 vilivyopokea vifaa tiba pamoja na kuchangia majanga yakiwemo ugonjwa wa Corona kwa kutoa TZS Milioni 400.Alisema kuwa Benki hiyo ina ATM 17 na Mawakala zaidi ya 100 huku akieleza azma ya Benki yake ya kuweka huduma za Kibenki za kutumia kadi za Kimataifa “Union Pay International” (UPI) katika uwanja mpya wa Abeid Amani Karume Zanzibar.

Halikadhalika, Bi Zaipuna alisema kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ina asilimia 31.8 za hisa katika benki hiyo.Sambamba na hayo, Mtendaji Mkuu huyo wa NMB alieleza kuwa Benki hiyo imeweza kujenga uwezo wa wakulima na wavuvi Zanzibar wakiwemo wakulima wa chumvi na mwani ambapo pia mikopo ya zaidi ya TZS Bilioni 3.9 imetolewa kwa zaidi ya wafanyabiashara 200 wadogo wadogo na wakati na zaidi ya wajasiriamali 500 wamefikiwa kupitia program endelevu ya kuwajengea uwezo.