RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema Sekta binafsi, ikiwemo biashara zimekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya mataifa mbali mbali Duniani.

Dk. Shein amesema hayo katika ufunguzi wa jengo jipya la skuli ya Sekondari ya Biashara iliopo Mombasa mjini hapa, ikiwa ni shamra shamra za maadhimisho ya miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Amesema mnamo mwaka 1980, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, iliondokana na mfumo wa kuhodhi biashara na badala yake kujikita katika usimamizi wa sera na sheria, ili kutoa fursa kwa wadau wa sekta hiyo kufanya shughuli hizo kwa mapana.

“Watu wa sekta binfasi ikiwemo biashara ndio wanaoimarisha nchi zao duniani kote, serikali haiwezi ikafanya kila kitu”, alisema.

Alisema hatua ya wafanyabiashara kurejesha faida kwa wananchi, hususan wanyonge, huleta baraka kubwa, akinasibisha kauli hiyo na hatua ya Mfanyabiashara Ahmada Yahya Abdulwakil aliefadhaili ujenzi wa jengo la skuli hiyo na kusema ni miongoni mwa wafanyabiashara weledi na wanaofanya vyema.

Alisema anawaheshimu wafanyabiashara ikiwemo wale wanaofanya vyema shughuli zao kw auadilifu na hatimae kurejesha faida kwa jamii, akibainisha kuwa biashara ni amali yenye heshima kubwa kwa Mwenyezi Mungu.

Dk. Shein alisisitiza umuhimu wa kuwaendeleza vyema wanafunzi wa skuli hiyo juu ya namna bora ya kufanya biashara ili waweze kulisaidia Taifa na kueleza kuwa Taifa linahitaji wataalamu wa kutosha katika masuala ya uchumi.

“Uzinduzi wa skuli hii ulete tija kubwa baadae kwa kutoa wataalamu wengi zaidi wa uchumi”, alisema.

Aidha, alisema mabadiliko yanayoendelea katika sekta ya elimu hapa nchini, kuanzia mwaka 1964 hadi sasa, yanalenga kuifikisha Zanzibar katika maendeleo makubwa ya kiuchumi na kijamii.

Alisema Zanzibar ni miongoni mwa nchi chache duniani zenye mfumo wa kutoa elimu bure, huku ikilenga kupanua wigo wa hatua hiyo hadi kufikia ngazi za Chuo Kikuu pale uchumi wake utakapoimarika.

“Kuna umuhimu wa kutafakari kwa kina vipi Serikali itaweza kufikia malengo hayo”, alisema.

Alisema kabla ya Mapinduzi ya Zanzibar ya 1964, elimu ilihodhiwa na wakoloni, ambapo ni wazalendo wachache wenye uwezo ndio waliopata fursa ya kusoma na kuliacha kundi kubwa la wazalendo bila ya kupata fursa hiyo.

Aidha, alisema elimu ilitolewa kwa ubaguzi kuambatana na makabila ya watu, hivyo Waafrika waliikosa fursa hiyo, hadi mwaka 1935 pale skuli ya mwanzo ilipoanzishwa kijiji cha Dole.

Rais Dk. Shein, alisema mara baada ya Mapinduzi ya 1964, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume kupitia manifesto ya ASP, alitangaza elimu bure nchini kote, hatua iliyotowa fursa kwa wananachi wote kusoma hadi kikomo cha uwezo wao.

Katika hatua nyengine Dk. Shein alimpongeza mfadhili wa ujenzi huo Ahmada Yahya Abdulwakil na kusema ni mfanyabiashara mzalendo, mkweli na muadilifu ambae amekuwa akitoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Zanzibar, hususan kupitia sekta ya elimu.

Mapema, Waziri wa Elimu na mafunzo ya Amali, Riziki Pembe Juma, alimpongeza mfanyabiashara huyo kwa uzalendo na juhudi kubwa anazochukuwa kuimarisha sekta ya elimu na kuwawekea mazingira bora ya masomo wanafunzi.

Aidha, alimpongreza Rais, Dk. Ali Mohamed Shein kwa kufungua milango ya uwekezaji kwa wazalendo na kuwa chachu ya maendeleo ya Taifa.

Nae, Mfanyabiashara Ahmada Yahya Abdulwakili ambae pia ni Mwakilishi wa kuteuliwa, alisema kwa kushirikiana na Serikali amefanikisha dhamira ya ujenzi wa jengo hilo ili kusaidia juhudi za Serikali katika kuondokana na uhaba wa madarasa unaozikabili skuli mbali mbali na kuwafanya wanafunzi kusoma katika mazingira bora.

Aliipongeza Serikali, ikiwemo viongozi na watendaji wa Wizara za Elimu na Mafunzo ya Amali pamoja na Wizara ya Fedha kwa mashirikiano makubwa yaliofanikisha kukamilika kwa ujenzi huo.

Aidha, alimshukuru Dk. Shein kwa kubainisha umuhimu wa wananchi, ikiwemo wafanyabiashara kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa Taifa lao.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Eng. Dk. Idriss Muslim alisema ujenzi wa jengo hilo linalohusisha ghorofa mbili, likiwa na madarasa tisa na ofisi mbali mbali za huduma za kitaaluma umegharimu zaidi ya shilingi Bilioni 1.1 hadi kukamilika kwake.

Alisema katika ujenzi huo Familia ya Mfanyabiashara Ahmada Yahya Abdulwakil imechangia shilingi Milioni 900, wakati ambapo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imechangia zaidi ya shilingi Milioni 263.

Alisema kukamilika kwa ujenzi wa jengo hilo kutaondoa mrundikano wa wanafunzi katika madarasa, kutoka wanafunzi 49 kwa darasa hadi kufikia 36 kupitia mkondo mmoja wa masomo.

Dk. Idriss aliwataka wadau wa elimu kote nchini kushirikiana ili kuzitafutia ufumbuzi changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta hiyo, sambamba na kuitaka jamii kuitunza skuli hiyo.