WAZEE wa CCM Wilaya ya Magharibi Unguja wameeleza kuridhishwa na uongozi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein ambaye pia, ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na kukiri kwamba anawatendea haki.
Kauli hiyo imetolewa kwa nyakati tofauti na wazee wa CCM wa Wilaya hiyo wakati walipokutana na Rais Dk. Shein huko katika ukumbi wa Afisi ya CCM Mkoa wa Mjini iliyopo Amani na ukumbi wa Manispaa ya Magharibi A, Kianga Mkoa wa Mjini Magharibi katika Mikutano aliyoindaa Rais Dk. Shein ambaye pia ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar kwa ajili ya wazee hao.
Katika hotuba yao wazee hao walikiri kuwa Rais Dk. Shein katika kipindi chake cha uongozi wa Awamu ya Saba amekuwa akiwatendelea haki katika kuleta maendeleo huku akiwa anasimamia vyema utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 sambamba na kustawisha huduma za jamii.
Walieleza kuwa katika Wilaya yao wamefaidika kwa mambo makubwa mno kama vile huduma za elimu bure ambapo tayri katika Wilaya yao wana skuli 6 za Ghorofa za Sekondari hivi sasa, huduma za miundombinu ambapo tayari kero za barabara ya Kibondemzungu na Mwanakwerekwe zimeshatatuka na hivi sasa zinapitika.
Aidha, walieleza kuwa barabara ya Kiembesamaki kuelekea Uwanja wa Ndege ambayo ilikuwa na tatizo la kutuwama maji wakati wa mvua tatizo ambalo limeshaondoka baada ya kutengenezwa mtaro mkubwa wa maji wa kisasa.
Waliongeza kuwa huduma za afya, maji safi na salama, umeme pamoja na huduma nyengine za kijamii zinapatikana bila ya wasi wasi katika Wilaya yao.
Wazee hao walitoa shukurani na pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kuendelea kuwajali mno ikiwa ni pamoja na kuwahudumia wao pamoja na wananchi wote kwa ujumla na kuamua kwa makusudi kuwatunza wazee kwa kuwapatia Pencheni Jamii.
Pamoja na hayo, wazee hao walimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuamua kufanya jambo hilo kubwa tena bila ya kuangalia itikadi ya kisiasa jambo ambalo limewaonesha upendo wake wa dhati kwa wananchi anaowaongoza na kueleza kuwa katika Wilaya yao, wastani wa wazee 1,663 wanalipwa kwa kila mwezi.
Katika hotuba yao hiyo wazee hao wa Wilaya ya Dimani walieleza kuwa kwa kufuata Ibara ya 5 kifungu cha (1) cha Katiba ya CCM inaeleza malengo na madhumuni ya chama hicho ni kushinda katika chaguzi zote.
Walieleza kuwa ushindi huo ni kwa ajili ya kushinda katika Uchaguzi wa Serikali Kuu na Serikali za Mitaa Tanzania Bara na Zanzibar ili kuunda na kushika Serikali Kuu na Serikali za Mitaa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania upande mmoja na Zanzibar upande wa Pili.
Hivyo, wazee hao walieleza mikakati waliyoiweka katika kuhakikisha chama chao cha CCM kinaendelea kushika hatamu na kuwaletea maendeleo wananchi wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Wakitoa taarifa yao wazee wa Wilaya ya Mfenesini walieleza kuwa wanaridhika na utendaji wake wa kazi katika vipindi vyake hajawaangusha lakini hiki cha pili ndio ametia for a zaidi katika utekelezaji wa Ilani ya CCM na kuwahudumia wananchi.
Walieleza kuwa mambo mengi na makubwa ameyafanya hata na sisi wazee wanafaidika na matunda ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar kama vile maji safi na salama, huduma za afya, elimu bure na skuli za kisasa za ghorofa ambazo zimejengwa katika Wilaya yao, mawasiliano na miundombinu bora ya umeme sambamba na Amani na utulivu uliopo.
Waiongeza kuwa jumla ya wazee 1534 wenye umri wa miaka 70 na kuendelea wananufaika na Pencheni Jamii sawa na TZS Milioni 30.6 kwa mwezi na TZS milioni 368.1 kwa mwaka.
Kwa kupitia Mabaraza ya Wazee yaliyoundwa na Chama pamoja na Serikali waliahidi kua wataendelea kuwa nae bega kwa bega na kuendelea kuiunga CCM na kuhakikisha kinaendelea kuwa madarakani.
Aidha, walieleza kuwa katika Wilaya yao wanacho kituo cha kutunzia wazee kilichopo Welezo ambacho kina Jumla ya Wazee 36 ambao wanawake 7 na wanaume 29 ambapo wanapatiwa huduma zote za Kijamii pamoja na posho ya kujikimu ya TZS elfu 40,000 kwa kila mmoja kwa mwezi sawa na TZS milioni moja na laki nne na arobaini elfu 1,440.000. ambapo kwa mwaka sawa na TZS Milioni 17,280.000.
Pamoja na hayo, wazee hao pia kupitia Mfukowa TASAF wa kusaidia Kaya Masikini baadhi ya Wazee nao wanafaidika kwa namna moja amanyengine ambapo yote hayo yanafanyika kwa upendo wake wa dhati kwa wazee.
Nae Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alisema kuwa wazee ni vyema wakasikilizwa kwani wana mambo mengi ambayo yatasaidia katika kukiimarisha chama hicho na hatimae kuendelea kupata ushindi katika chaguzi zake zote.
Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imewaweka wazee katika programu zake zote za maendeleo ukiwemo Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini (MKUZA) na mipango mengineyo ya kiuchumi kwa lengo la kuendelea kuwatunza.
Alisisitiza kuwa CCM ina kila sababu ya kuwatunza na kuwaenzi wazee na kuwataka viongozi wa chama hicho kuwa karibu na wazee na kuchukua maoni yao pale wanapoyahitaji.
Alisema kuwa ni vyema viongozi wa Chama hicho ukawatumia wazee katika shughuli zao za kichama hasa ikizingatiwa kwamba Chama hicho kina mtandao mkubwa wa uongozi.
Rais Dk. Shein alisema kuwa wazee wanayajua mambo mengi na wana historia kubwa ya kabla na baada ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 hivyo, ni vyema wakathaminiwa kwani Mapinduzi ndiyo yaliyomkomboa mnyonge.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa kuna kila sababu ya kuulinda, kuuenzi na kuutunza Muungano wa Tanganyika na Zanzibar hasa ikizingatiwa kwamba Zanzibar inafaidika kwa kiasi kikubwa na Muungano huo.
Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa kuwepo kwa wazee imara na uongozi madhubuti wa CCM ndio utakaopelekea ushindi wa chama hicho.
Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alieleza haja kwa wazee kuwaeleza vijana jinsi ya kuwaheshimu na kuwathamini wazee kwani wazee ndio kila kitu.
Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini na inazijali juhudi walizozichukua wazee hadi kupatikana kwa uhuru wa Tanganyika na Zanzibar.
Katika hotuba yake aliyoitoa mbele ya wazee hao wa CCM pamoja na viongozi wengine wakuu wa chama hicho Rais Dk. Shein alieleza kuvutiwa na taarifa yao waliyoisoma ambayo imeonesha jinsi wazee wa Wilaya hiyo walivyoweka mikakati ya kukiimarisha chama chao ili kiendelee kupata ushindi wa kishindo.
Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Abdalla Juma Mabodi alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa azma yake ya kukutana na wazee na kuupongeza utamaduni wake wa kukutana na wanachama wa ngazi za chini wa chama hicho wakiwemo wazee.
Alieleza kuwa CCM imeanza muda mrefu kuwathamini wazee kwani Baraza la Wazee ndio ngome madhubuti ya chama hicho kwani Baraza la asili la Wazee wa Ofisi Kuu ya CCM Kisiwandui ambalo limeundwa siku ya pili baada ya kuundwa chama cha ASP.
Alisema kuwa katika miaka tisa ya uongozi wake mambo mengi ameyafanya Rais Dk. Shein kutokana na hikma na uzalendo wake mkubwa wa kuendesha Serikali na Chama hali ambayo imeleta maendeleo makubwa sambamba na amani na utulivu nchini.
Nao Wenyeviti wa CCM Wilaya ya Dimani na Wilaya ya Mfenesini Kichama walieleza kuwa mafanikio makubwa yamepatikana katika Awamu ya Saba inayoongozwa na Rais Dk. Shein huku wakisema kuwa mashirikiano makubwa yamepatikana kati ya viongozi wote wa Chama, Serikali pamoja na wanachama wa chama hicho.
Aidha, Wenyeviti hao walieleza kuwa kutokana na miongozo, maelekezo na uongozi mzuri wa Makamo Mwenyekiti wa Chama hicho, Rais Dk. Shein mafanikio makubwa yanaendelea kupatikana kutokana na utekelezaji wake mzuri wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020.