HOTUBA YA RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI MHESHIMIWA DK. HUSSEIN ALI MWINYI, KATIKA MAADHIMISHO YA MIAKA 61 YA MAPINDUZI MATUKUFU YA ZANZIBAR

TAREHE: 11 JANUARI, 2025

Assalamu aleikum

Naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutujaalia uhai na afya njema na kutuwezesha kuifikia siku ya leo, ambapo wananchi wa Zanzibar tunaungana na Watanzania wote katika mkesha wa Maadhimisho ya Miaka 61 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964.

Kwa hakika, Mapinduzi ya mwaka 1964 ni tukio muhimu la historia ya nchi yetu ambapo wazee wetu wakiongozwa na Jemedari wa Mapinduzi Mzee Abeid Amani Karume walijitoa muhanga ili kuikomboa nchi yetu na kufungua ukurasa mpya wa maendeleo yetu. Tunamuomba Mwenyezi Mungu awarehemu waasisi wetu wa Mapinduzi, Viongozi na wananchi wenzetu waliotangulia mbele ya haki.

Ndugu Wananchi,

Kuanzia tarehe 20 Disemba, 2024, tulianza shughuli mbali mbali za kuadhimisha miaka 61 ya Mapinduzi kote Unguja na Pemba tukiwa na kauli mbiu isemayo: Miaka 61 ya Mapinduzi, Amani, Umoja na Mshikamano kwa Maendeleo yetu. Nachukua fursa hii kuwashukuru wananchi kwa kuifasiri kauli mbiu hiyo kwa vitendo na kujitokeza kwa wingi katika matukio mbali mbali yaliyoandaliwa, kwa ajili ya sherehe za Maadhimisho ya Miaka 61 ya Mapinduzi. Ni matarajio yangu kuwa na kesho siku ya kilele, mtajitokeza kwa wingi katika Uwanja wa Gombani ili kuhitimisha sherehe zetu.

Ndugu Wananchi,

Miaka 61 ya mafanikio ambayo nchi yetu imeyapata, msingi wake ni Mapinduzi Matukufu ya Mwaka 1964 pamoja na jitihada za wananchi na viongozi wa awamu zote zilizotangulia. Serikali ya Awamu ya Nane ilipoingia madarakani miaka minne iliyopita, imefanya juhudi za kuyaendeleza mafanikio yaliopatikana na kuhakikisha Zanzibar inazidi kupiga hatua za maendeleo katika sekta zote pamoja na kudumisha misingi ya amani, uzalendo na umoja wa kitaifa.

Aidha, wakati nikizindua Baraza la Wawakilishi mwaka 2020, nilibainisha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Nane ya kuyadumisha malengo ya Mapinduzi kwa kuleta mageuzi ya kiuchumi ili kuongeza kasi ya maendeleo na ustawi wa maisha ya wananchi wa Zanzibar. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa mafanikio ambayo tunaendelea kuyapata ya kuifikia dhamira hiyo katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Nane.

Ndugu Wananchi,

Tunapoadhimisha miaka 61 ya Mapinduzi tunafurahia mafanikio makubwa tuliyoyapata katika kudumisha amani, umoja na mshikamano pamoja na hatua  tulizofikia katika kukuza uchumi, ujenzi wa miundo mbinu, uwekezaji na biashara, kuboresha huduma za jamii na kuimarisha demokrasia na utawala bora.

Uchumi wa Zanzibar umeendelea kuimarika ambapo hadi kufikia mwezi Septemba mwaka 2024, uchumi umekua kwa kasi ya asilimia 7.5. Pato la Taifa kwa bei za soko (GDP at current price) nalo limeongezeka kufikia thamani ya TZS trilioni 6.04 mwaka 2023 kutoka TZS trilioni 4.78  mwaka 2021 ambayo ni sawa na ongezeko la asilimia 26. 

Kuongezeka kwa Pato la Taifa na Kasi ya Ukuaji wa Uchumi kumesababishwa na kuimarika kwa  Sekta ya Huduma iliyokuwa kwa wastani wa asilimia 9.9 mwaka 2023 kutoka wastani wa asilimia 1.3 mwaka 2021. Sekta ndogo ya huduma za watalii imeimarika zaidi, watalii waliotembelea Zanzibar wameongezeka kwa asilimia 145 kwa kipindi hicho. Kadhalika, kuongezeka kwa ukusanyaji wa Mapato ya Serikali kwa asilimia 51 kutoka TZS bilioni 858.2 mwaka 2020/2021 kufikia Shilingi trilioni 1.3 mwaka 2022/2023.

Hali ya Mfumko wa bei imeendelea kudhibitiwa na kubaki katika tarakimu moja. Hali ya mfumko wa bei imekuwa ya kupanda na kushuka kutokana na kuongezeka kwa bei za bidhaa na huduma katika soko la Dunia. Kwa Zanzibar kasi ya mfumko wa bei ilipungua hadi asilimia 4.5 mwezi Novemba, 2024.

Ndugu Wananchi,

Tunafurahia mafanikio makubwa yaliyopatikana katika jitihada zetu za kuvutia wawekezaji. Kasi ya uwekezaji nchini imeongezeka ambapo jumla ya miradi 449 yenye thamani ya Dola za kimarekani  bilioni 5.9 imesajiliwa na Mamlaka ya Vitega Uchumi Zanzibar, inayotarajiwa kuzalisha ajira zaidi ya 22,966. Miradi hiyo inahusisha uwekezaji katika sekta ya hoteli yenye jumla ya miradi 169, biashara za majengo miradi 99, viwanda miradi 43, kilimo miradi 28, michezo miradi 28 na sekta nyenginezo miradi 82.

Kwa lengo la kuimarisha uwekezaji katika sekta ya uchumi wa buluu, Serikali kupitia ZIPA imeruhusu uwekezaji katika visiwa vidogo vidogo. Hadi sasa, ZIPA imesajili miradi ya uwekezaji katika visiwa kumi na saba, ambapo jumla ya Dola za Kimarekani milioni 377.5 zinatarajiwa kuwekezwa. Aidha, Serikali inaendelea kuchukua hatua za kuvutia wawekezaji na kutangaza fursa zilizopo katika maeneo ya Bandari Jumuishi ya Mangapwani, huku ujenzi wa miundombinu ya barabara, maji na umeme kwa ajili ya maeneo ya uwekezaji ukiendelea.

Ndugu Wananchi,

Kwa lengo la kuleta Mapinduzi ya kiuchumi, Serikali inaendelea na hatua za kuwawezesha wananchi kiuchumi ili kupambana na umasikini. Mafanikio yanaendelea kupatikana katika utekelezaji wa dhamira hiyo ya Serikali. Jumla ya mikopo yenye thamani ya TZS bilioni 35.2 imetolewa na Wakala wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi kwa wananchi 24,111 wakiwemo watu wenye ulemavu 373. Mikopo hiyo, imetolewa kwa sekta mbali mbali zikiwemo biashara, kazi za mikono, ujenzi, kilimo na ufugaji. Kati ya wanufaika wa mikopo hiyo, asilimia 40 ni vijana. Aidha, Serikali imetoa TZS bilioni 60 kwa ajili ya kuwanufaisha wajasiriamali.

Ndugu Wananchi,

Katika kuwapatia mazingira bora ya kufanyia shughuli zao wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo, Serikali imekamilisha ujenzi wa masoko makubwa ya Mwanakwerekwe na Jumbi ambapo mwezi Novemba, 2024 nimeyazindua. Kukamilika kwa masoko hayo, kumewawezesha zaidi ya wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo 7,000 kufanya shughuli zao katika mazingira mazuri na ya kudumu. Napenda kuwajulisha wananchi kuwa soko la Chuini pamoja na kituo cha mabasi kilichopo katika eneo hilo, tunatarajia kulifungua mapema mwaka huu wa 2025. Aidha, Serikali imeendelea na ujenzi wa masoko madogo katika Mikoa na Wilaya zote Unguja na Pemba kwa madhumuni ya kuimarisha mazingira ya biashara ili kuepuka kufanya biashara katika maeneo yasiyo rasmi.

Ndugu Wananchi,

Kwa upande wa sekta ya viwanda, jitihada za kuvutia uwekezaji katika viwanda nchini zimepata mafanikio. Katika kipindi hiki, juhudi zaidi zimewekwa katika uimarishaji wa miundombinu ikiwemo barabara, umeme na huduma za maji safi na salama katika maeneo yanayolengwa kuanzishwa viwanda. Jumla ya TZS bilioni 33.122 zimetumika kwa ujenzi wa miundombinu katika eneo la Dunga Zuze. Jitihada za kuvutia uwekezaji katika eneo hilo  zimefanikiwa ambapo tayari Serikali imeshatoa hati za ukodishaji wa ardhi (Sub lease) kwa wawekezaji saba (7).

Wawekezaji hao wataanzisha ujenzi wa viwanda vikiwemo; viwanda vya  kutengeneza dawa za binaadamu viwili, kiwanda cha kuunganisha pikipiki, bajaji na gari zinazotumia umeme. Chengine ni kiwanda cha kuzalisha bidhaa mbali mbali za plastic pamoja na kiwanda cha kuzalisha nguo. Aidha, uwekezaji mwengine ni wa kiwanda cha kuzalisha bidhaa za chuma, pamoja na ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme wa jua MW50 utakaotumika katika eneo la Dunga na wa ziada utaingizwa katika gridi ya Taifa.  Ni matarajio yetu kuwa kukamilika kwa miradi hiyo kutazidi kuimarisha mchango wa sekta ya viwanda katika Pato la Taifa kutoka asilimia 20.8 ya sasa na kufikia asilimia 25 mwaka 2030, pamoja na kuchangia upatikanaji wa ajira, bidhaa na kuchochea kuimarika biashara nchini.

Ndugu Wananchi,

Tunapoadhimisha miaka 61 ya Mapinduzi mafanikio makubwa yamepatikana katika sekta kuu za uchumi wa buluu ambazo ni uvuvi na ufugaji wa mazao ya baharini, ukulima wa mwani, utalii, bandari na biashara zinazohusiana na usafiri wa majini pamoja na mafuta na gesi asilia.

Utalii ni sekta iliyopewa mazingatio zaidi kutokana na mchango wake katika kutupatia fedha za kigeni na ajira.  Tunapoadhimisha miaka 61 ya Mapinduzi mafanikio makubwa yamepatikana katika sekta hii kwa kuongezeka kwa idadi ya watalii na kuimarika kwa sekta ya huduma hapa nchini. Idadi ya watalii walioingia nchini imeongezeka kutoka watalii 568,312 katika mwezi Novemba 2023 na kufikia watalii 645,144 katika mwezi Novemba 2024. Idadi hiyo ni sawa na ongezeko la asilimia 14.

Ndugu Wananchi,

Katika utekelezaji wa Sera ya Uchumi wa Buluu, Serikali imefanya jitihada kubwa katika kuimarisha sekta ya uvuvi na ukulimawa  mazao ya baharini ili kuongeza tija katika shughuli hizi na kuchangia ukuaji wa uchumi. Serikali imewapatia wananchi mbinu bora za kutekeleza shughuli zao, vifaa vya kufanyia kazi pamoja na ujenzi wa madiko na masoko ya kuuzia samaki ili wawe na mazingira mazuri ya kufanyia kazi. Jumla ya boti 1,027 za uvuvi na kilimo cha mwani zimetolewa na kuwanufaisha wananchi 32,000 kati yao asilimia 70 ni vijana na asilimia 90 ya boti za ukulima wa mwani wanufaika wake ni wanawake.

Katika kuimarisha miundimbinu ya uvuvi, Serikali ilikamilisha ujenzi wa diko la samaki la kisasa la Malindi ambalo limeanza kutumika likihudumia wastani wa watu 10,000 na boti za uvuvi 350 kwa siku. Ujenzi wa madiko na masoko mengine ya samaki umeanza katika maeneo ya Mkoani Pemba na Fungurefu Unguja. Pia, Serikali inaendelea na ujenzi wa viwanda vya kuongezea thamani dagaa eneo la Kama Unguja na Ndagoni Pemba sambamba na matayarisho ya ujenzi wa bandari mbili za uvuvi katika eneo la Ngalawa Unguja na Shumba Mjini kwa Pemba pamoja na ujenzi wa kiwanda cha kuchakata samaki katika eneo la Fungurefu Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Jitihada za Serikali, zimechochea kuongezeka kwa uzalishaji wa samaki wanaovuliwa kwa asilimia 107.2 kutoka tani 38,107 mwaka 2020 zenye thamani ya TZS bilioni 205.35 hadi kufikia tani 78,943 mwaka 2024 zenye thamani ya TZS bilioni 618.18. Serikali itaendelea kuwasaidia wavuvi ili kuwajengea uwezo wa kufanya shughuli zao kwa tija ikiwemo kuwapatia vifaa, mikopo na utaalamu ili wavue kisasa na kufika bahari kuu, pamoja na kuwajengea miundombinu bora ya shughuli za uvuvi.

Ndugu Wananchi,

Kwa upande wa kilimo cha mwani, jitihada zilizofanywa za kuimarisha ukulima huo kwa kuwapa vifaa, taaluma na kuwajengea mazingira bora wakulima wa mwani zimepata mafanikio. Ujenzi wa kiwanda cha kusarifu mwani Chamanangwe Pemba umekamilika. Hatua za kuweka mitambo ya kiwanda hicho kwa ubia kati ya Serikali na Kampuni ya Nutri-San ya Uingereza zinaendelea ambapo uzalishaji unatarajiwa kuanza kati kati ya mwaka huu wa 2025. Kiwanda hiki kitakuwa na uwezo wa kuchakata tani 30,000 za mwani mkavu kwa mwaka na kitakapoanza kazi, kitachochea uzalishaji  wa zao la mwani na kuwa na soko la uhakika la zao hili. Kwa wastani ukulima wa mwani unatoa ajira kwa watu wapatao 16,000 ambapo asilimia 80 ni wanawake. Mafanikio yamepatikana ya kuimarisha kilimo cha mwani ambapo uzalishaji wa zao hilo umeongezeka kwa asilimia 124.6 kutoka tani 8,785 zenye thamani ya TZS bilioni 5.39 mwaka 2020 na kufikia tani 19,716 zenye thamani ya TZS bilioni 16.14 mwaka 2024.

Ndugu Wananchi,

Kuwepo kwa bandari na usafiri wa majini kuna umuhimu mkubwa katika uchumi wa nchi za visiwa kama ilivyo Zanzibar. Tunapoadhimisha miaka 61 ya Mapinduzi jitihada kubwa zimefanywa na Serikali katika kuimarisha huduma za bandari zetu na usafiri wa majini. Kwa upande wa bandari, Serikali ilifunga mkataba na Kampuni ya Africa Global Logistic (AGL) ili kusimamia uendeshaji wa bandari ya Malindi kwa jina la Zanzibar Multipurpose Terminal (ZMT).

Hatua hii imeleta mageuzi makubwa ya huduma za bandari ya Malindi ambapo idadi ya siku za kuegesha meli zimepungua kutoka 7 hadi 4 kutokana na uboreshaji mkubwa uliofanywa na matumizi ya vifaa na teknolojia ya kisasa. Uwezo wa kuhudumia kontena umeongezeka kufikia makontena 70,768 mwaka 2024, sawa na asilimia 67 ya malengo ya kuhudumia makontena 105,000 kwa mwaka 2025. Hatua ya ujenzi wa bandari kavu ya Maruhubi na kuanza kutumika kutachochea kuongeza ufanisi katika huduma za bandari. Vile vile, Serikali kwa kushirikiana na mwekezaji imeanzisha bandari ya mizigo katika eneo la Fumba na kuimarisha bandari ya Mkoani Pemba ambayo kwa sasa imeanza kutoa huduma za kupokea  meli za makontena kutoka nje ya nchi.

Ndugu Wananchi,

Hivi sasa Serikali inaendelea na maandalizi ya ujenzi wa bandari ya mizigo katika eneo la Mangapwani. Aidha, ujenzi wa miundombinu ya barabara katika eneo la bandari hiyo umefikia asilimia 40 ambapo tayari km 5.8  kati ya km 12 ya barabara imeshawekwa lami ngumu. Katika eneo hili jumla ya nyumba 247 zinaendelea kujengwa kati ya nyumba 370 zitakazojengwa kwa ajili ya fidia kwa wananchi waliopisha mradi huu.

Aidha, Ujenzi wa Bandari ya Shumba Mjini unaendelea na umefikia asilimia 65 ya utekelezaji na eneo la ujenzi wa Bandari ya Kizimkazi limeshapimwa kwa matayarisho ya awali ambapo ujenzi unatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwaka huu wa 2025. Sambamba na hayo, Serikali imefunga mkataba na kampuni ya ZF DEVCO kwa ajili ya ujenzi wa Bandari ya abiria  katika eneo la Maruhubi. Mradi huo utakaojumuisha ujenzi wa jeti na ghala la kuhifadhia mizigo una lengo la kuimarisha usafiri wa baharini.

Ndugu Wananchi,

Kwa lengo la kuimarisha usafiri wa baharini, Serikali imeingia mkataba na Kampuni ya Synergy Ship Builders ya India kwa ajili ya ujenzi wa boti 2 za mwendo wa kasi zitakazofanya kazi baina ya bandari ya Unguja, Pemba, Tanga na Dar es Salaam. Ujenzi wa boti hizo za kisasa unatarajiwa kuanza rasmi mwezi Februari, 2025.  Nachukua fursa hii kuwashukuru kwa dhati wadau wenzetu wa sekta binafsi Kampuni ya Azam Marine na Zan Fast Farries kwa mchango wao katika kusaidia kukabiliana na changamoto hii kwa kuimarisha usafiri kati ya bandari za Unguja, Pemba, Dar es Salaam na Tanga.

Juhudi zinazochukuliwa za kuimarisha usafiri wa baharini, zimewezesha kuongezeka kwa idadi ya abiria wanaotumia usafiri huo pamoja na vyombo vya baharini. Idadi ya abiria wanaotumia usafiri wa bahari wakiwemo wageni na watalii wamefikia 5,000 hadi 7,000 kwa siku idadi ambayo hatujawahi kufikiwa. Aidha, jumla ya meli 675 za abiria na mizigo zimesajiliwa Zanzibar. 

Ndugu Wananchi,

Ujenzi wa miundombinu ni hatua muhimu katika kuchochea kasi ya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya nchi. Katika miaka 61 ya Mapinduzi juhudi kubwa imefanywa na Serikali katika ujenzi wa barabara na uimarishaji wa viwanja vya ndege. Mafanikio makubwa yamepatikana katika ujenzi wa  barabara za mjini na barabara za ndani nchini. Hadi mwezi Disemba, 2024, Serikali imekamilisha ujenzi wa km 73.83 kati ya km 100.9 za mjini kwa kiwango cha lami na zege. Utekelezaji wa mradi huu umefikia asilimia 68 na unajumuisha ujenzi wa madaraja ya juu mawili (flyover) ambapo Mwanakwerekwe umefikia asilimia 80 na Amani asilimia 50. Kuhusu barabara za ndani hadi mwezi Disemba, 2024, jumla ya km 66.49 kati ya km 275.9 za barabara kwa kiwango cha lami zimekamilika, sawa na asilimia 24.10 ya utekelezaji.

Katika  mwaka uliopita, Serikali imefanikiwa kukamilisha ujenzi wa barabara ya Jozani – Charawe – Ukongoroni – Bwejuu yenye urefu wa km 23.3 kwa kiwango cha lami na kuondoa changamoto ya usafiri wa barabara iliyowakabili wananchi wa vijiji hivyo kwa muda mrefu. Aidha, kazi ya ujenzi wa daraja la Uzi – Ng’ambwa na barabara yenye urefu wa km 8.73 imeshaanza. Kadhalika, ujenzi wa barabara kuu km 277 Unguja na Pemba umeanza. Kuhusu ujenzi wa barabara ya Tunguu – Makunduchi km 48, Fumba – Kisauni km 12 na Chake chake – Mkoani km 43.5, Serikali inakamilisha maandalizi na ujenzi wake na unatarajiwa kuanza karibuni. Aidha, ujenzi wa barabara ya Wete – Chake chake km 22.1 unaendelea ambapo hadi kufika Disemba 2024, jumla ya km 18 zimekamilika  kwa kiwango cha kifusi na km 11 tayari zimewekwa lami. Mradi huu umefikia asilimia 42 ya utekelezaji wake.   

Ndugu Wananchi,

Tunapoadhimisha miaka 61 ya Mapinduzi mafanikio makubwa yamepatikana katika kuimarisha huduma za viwanja vya ndege na usafiri wa anga. Mageuzi makubwa yaliyofanywa na Serikali ya kushirikisha sekta binafsi, yamewezesha mapato ya Mamlaka ya viwanja vya ndege kuongezeka kutoka TZS bilioni 11.6 mwaka 2019/2020 na kufikia TZS bilioni 40.2  mwaka 2023/2024, pamoja na kuimarika kwa huduma za wasafiri. Idadi ya abiria wanaotumia viwanja vyetu vya ndege wameongezeka kutoka abiria 1,305,222  mwaka 2021 na kufikia abiria 2,140,986 mwaka 2024. Jumla ya mashirika ya ndege 81 ya kimataifa yanafanya safari zao moja kwa moja kuja Zanzibar na kupelekea kiwanja cha ndege cha AAKIA kupokea idadi kubwa ya abiria kwa mwaka kuliko viwanja vyote vyengine vya ndege nchini Tanzania.

Ndugu Wananchi,

Kwa lengo la kuimarisha huduma za viwanja vya ndege na usafiri wa anga, Serikali inafanya matengenezo makubwa ya jengo la abiria la Terminal One yanayotegemewa kukamilika mwezi Februari 2025 pamoja na kuendeleza ujenzi wa jengo jipya la abiria la Terminal Two. Ujenzi wa jengo jipya la abiria la Terminal Two litakalokuwa na uwezo wa kuhudumia zaidi ya abiria 1,400,000 kwa mwaka unakwenda pamoja na ujenzi wa maegesho ya gari 200 kwa wakati mmoja. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mwaka 2025, ukigharimu USD milioni 34. Hatua hii itaimarisha uwezo wa uwanja wa ndege wa AAKIA wa kuhudumia abiria zaidi ya 3,000,000 kwa mwaka na kuongeza ufanisi. Aidha, hatua ya ujenzi wa kituo cha biashara (Business Centre) katika jengo la Terminal Three kwa ushirikiano na Kampuni ya East Africa Developer Ltd kutaimarisha huduma na kuongeza haiba katika uwanja wa ndege wa AAKIA. Kuhusu ujenzi wa uwanja wa ndege wa Pemba, Serikali imekamilisha matayarisho pamoja na malipo ya awali. Kazi ya uwekaji vifaa vya ujenzi katika eneo la kazi, matayarisho na ulipaji wa fidia kwa wananchi watakaopisha mradi huo inaendelea. 

Ndugu Wananchi,

Tunapoadhimisha miaka 61 ya Mapinduzi mafanikio yanaendelea kupatikana katika kuimarisha upatikanaji wa huduma za umeme.Serikali ilifanya uamuzi wa kupunguza bei ya kuunganisha umeme kwa wananchi kwa wastani wa asilimia 50. Punguzo hilo ni kutoka TZS 464,000 hadi TZS 200,000 kwa gharama za uungaji usiozidi mita 30. Vile vile, kutoka TZS Mil. 1,700,000 hadi TZS 690,000 kwa gharama za uungaji wa nguzo moja na kutoka TZS Mil. 2,600,000 hadi TZS Mil.  1,040,000 kwa gharama ya uungaji wa nguzo mbili. Hatua hii pamoja na mageuzi makubwa yaliyofanywa na Serikali katika Shirika la Umeme, kumeimarisha upatikanaji wa huduma ya umeme kwa kuongezeka kwa idadi ya wananchi walioungiwa umeme pamoja na kuongeza usambazaji wa huduma hiyo. Hadi mwezi Julai 2024, jumla ya wateja wapya wa umeme 115,242 wameunganishiwa huduma. Aidha, Serikali imefanikiwa kupeleka huduma za umeme katika vijiji 222 kati ya Novemba, 2020 hadi Agosti, 2024. Kiwango hicho ni sawa na asilimia 72 ya lengo la kuunganisha vijiji 305 vilivyokusudiwa kufikishiwa huduma hiyo. 

Katika kuhakikisha Zanzibar inakuwa na huduma za uhakika za uzalishaji wa umeme, Serikali kupitia ZECO inaendelea kusimamia utekelezaji wa miradi ya kuzalisha umeme kwa nishati ya jua kwa ushirikiano na Kampuni ya Generation Capital Ltd ambayo kwa awamu ya kwanza itazalisha MW 30 za umeme katika eneo la Bambi. Kwa upande wa Pemba kampuni ya ESR itazalisha MW 15 za umeme wa jua eneo la Micheweni. Miradi hiyo, inatarajiwa kukamilika mwaka 2025. Aidha, Serikali inaendelea na utekelezaji wa mradi wa ZESTA ambao utazalisha MW 18 za umeme wa jua pamoja na mfumo wa kuhifadhia umeme wenye uwezo wa kuhifadhi MW 40.

Ndugu Wananchi,

Elimu ni moja ya Vipaumbele vya Serikali katika awamu zote za uongozi baada ya Mapinduzi kwa kuzingatia umuhimu wake katika kuandaa nguvu kazi ya Taifa.  Tunapoadhimisha miaka 61 ya Mapinduzi mafanikio makubwa yamepatikana nchini kutokana na mageuzi makubwa yaliyofanywa na Serikali kwa lengo la kuimarisha sekta ya elimu.

Hatua zilizochukuliwa na Serikali ni pamoja na kuimarisha miundombinu ya elimu kwa ujenzi wa Skuli mpya za ghorofa zenye miundombinu ya kisasa ya maabara, maktaba pamoja na vymba vya kompyuta na kufanya ukarabati wa Skuli za zamani. Jumla ya madarasa mapya 2,773 yamejengwa katika kipindi cha miaka minne kupitia ujenzi wa Skuli 35  za ghorofa. Idadi hiyo ni sawa na ongezeko la asilimia 184.8 ya malengo ya Ilani ya CCM 2020 ya kujenga madarasa 1,500. 

Kwa mwaka huu wa fedha 2024/2025, Serikali inalenga kujenga madarasa 2,037 ambapo ujenzi wake umeshaanza kupitia ujenzi wa Skuli mpya 79 zikiwemo 53 za chini na 26 za ghorofa. Lengo la Serikali ni kumaliza kabisa changamoto ya wanafunzi kuingia kwa shifti katika Skuli zetu na kuondoa msongomano wa wanafunzi madarasani. 

Ndugu Wananchi,

Serikali imeweka mazingatio katika kuimarisha miundombinu yenye kuwajengea vijana ujuzi na maarifa katika fani mbali mbali za ajira. Hivi sasa tumeanza mchakato wa ujenzi wa vyuo vitano vya mafunzo ya amali, chuo cha ubaharia na ujenzi wa karakana 33 zitakazojengwa katika Skuli tatu za Sekondari katika kila Wilaya. Hatua hii ni kujiandaa na mabadiliko ya mitaala ya Sekondari inayotarajiwa kuanza kutumika mwaka huu wa 2025.

Katika kuhakikisha, dhamira ya Serikali ya kuimarisha sekta ya elimu inafanikiwa, bajeti ya elimu imeongezwa kutoka TZS bilioni 265.5 mwaka 2021/2022 hadi TZS bilioni 830 mwaka 2024/2025, sawa na ongezeko la asilimia 212.6.

Uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika elimu, umeweza kuleta mafanikio ya kuongezeka kiwango cha ufaulu wa wanafunzi katika mitihani yao ya Taifa. Takwimu zinaonesha kuwa ufaulu katika mitihani ya kidato cha Nne umeongezeka kutoka asilimia 56.1 mwaka 2020 hadi asilimia 85.7 mwaka 2023. Matokeo ya mtihani wa kidato cha sita ya mwaka 2024 yanaonesha mafanikio makubwa zaidi ambapo asilimia 99.6 ya watahiniwa wamepata ufaulu wa kujiunga na vyuo vikuu. Katika kuhakikisha wanafunzi wote wenye sifa ya kujiunga na elimu ya Juu wanapata fursa hiyo, Serikali imeongeza bajeti ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya juu kutoka TZS bilioni 11.5 mwaka 2021/2022 hadi TZS bilioni 33.4 mwaka 2024/2025. Ongezeko hilo limewawezesha vijana wanaonufaika na mikopo ya elimu kuongezeka kutoka 4,289 hadi 6,060 wakiwemo vijana wa ngazi ya stashahada (Diploma).

Ndugu Wananchi,

Serikali inahakikisha ujenzi wa Skuli mpya zinazojengwa umezingatia kuwepo kwa vymba vya kompyuta, projekta na huduma ya uhakika ya intanenti ili kwenda sambamba na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Aidha, Serikali imeanza kuziunganisha Skuli na mkonga wa Taifa ili kuimarisha upatikanaji wa huduma za mtandao.Katika kukabiliana na changamoto ya uhaba wa walimu hasa wa masomo ya sayansi, Serikali imeajiri walimu wapya 3,531 ambapo katika mwaka huu wa fedha 2024/2025 ilipanga kuajiri walimu 1,867. 

Ndugu Wananchi,

Katika kipindi cha miaka 61 ya Mapinduzi juhudi kubwa imefanywa na Serikali katika kuimarisha huduma za afya nchini. Mageuzi makubwa yamefanywa katika muundo wa uendeshaji wa huduma za afya. Serikali imeimarisha miundombinu ya afya kwa kujenga hospitali kumi (10) za kisasa za Wilaya na moja ya Mkoa wa Mjini Magharibi zenye huduma bora za tiba zikiwemo za kibingwa pamoja na vifaa vya kisasa vya uchunguzi wa maradhi. Kuwepo kwa hospitali hizi kumefungua ukurasa mpya wa upatikanaji wa huduma za afya hapa nchini pamoja na kuboresha mfumo wa rufaa katika sekta ya afya.

Kwa lengo la kuimarisha huduma za afya katika ngazi ya msingi, Serikali imeanza ujenzi wa vituo vya afya kumi (10)  na dispensari 35. Kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China, Serikali imekamilisha ujenzi wa nyumba za kuhudumia familia 75 katika Hospitali ya Abdalla Mzee. Aidha, ujenzi wa nyumba za wafanyakazi katika hospitali za Wilaya Mwera Pongwe, Pangatupu na Kitogani kwa Unguja na Vitongoji na Kinyasini kwa Pemba zenye uwezo wa kukaa familia 16 kwa kila moja upo katika hatua za mwisho. Lengo ni kuwezesha watumishi wa sekta ya afya kuwa na mazingira mazuri ya kutekeleza majukumu yao.

Ndugu Wananchi,

Hali ya  upatikanaji wa dawa na vifaa tiba katika vituo vya afya vya Serikali na hospitali imeimarika kutokana na kuongezeka kwa bajeti ya dawa kutoka TZS bilioni 17 mwaka 2020/2021 hadi TZS bilioni 40 mwaka 2024/2025. Upatikanaji na usambazaji wa dawa umeimarika kutoka asilimia 65.5 mwaka 2020 hadi asilimia 95 katika hospitali za Wilaya na asilimia 74 katika Vituo vya afya kwa mwaka 2024. Aidha, Serikali imeimarisha nguvu kazi ya sekta ya afya kwa kuongeza idadi ya watumishi wa kada mbali mbali walioajiriwa, kutoka 559 mwaka 2020/2021 hadi kufikia 2,008 mwaka 2023/2024. Vile vile, watumishi 497 hivi sasa wapo masomoni wakiwemo madaktari bingwa 84, wauguzi bingwa 45 na madaktari wa ngazi ya digrii 128. Vile vile, watumishi 191 wakiwemo madaktari bingwa 19, wauguzi 46, wataalamu wa ganzi na usingizi 11 na wataalamu wengine wa ngazi ya digrii wamerudi masomoni na wanatarajiwa kuongeza nguvu katika jitihada za Serikali za kuimarisha huduma za afya.

Aidha, Sekta ya afya imefanikiwa kuongeza kiwango cha chanjo kwa watoto chini ya miaka mitano kutoka asilimia 83 mwaka 2020/2021 hadi asilimia 95 mwaka 2023/2024. Mafanikio haya yanatokana na juhudi za Serikali kuleta mageuzi katika huduma za afya kwa kushirikiana na sekta binafsi, hatua ambayo imeleta manufaa makubwa kwa wananchi.

Ndugu Wananchi,

Upatikanaji wa huduma za maji safi na salama kwa wananchi kumepewa kipaumbele. Serikali imeendelea kuimarisha uzalishaji, uhifadhi na usambazaji wa huduma za maji safi na salama kwa wananchi wanaoishi mijini na vijijini Unguja na Pemba.

Serikali imefanikisha utekelezaji wa miradi miwili mikubwa ya maji ambayo ni Mradi wa Uhuishaji na Uimarishaji wa huduma za Maji Zanzibar wenye thamani ya USD Milioni 92.18 na Mradi wa Uimarishaji Huduma za maji wa Fedha za Ahueni ya UVIKO-19 wenye thamani ya TZS bilioni 40.2. Kupitia Mradi wa Uhuishaji na Uimarishaji Huduma za Maji, jumla ya matangi 15 yenye uwezo wa kuhifadhi lita milioni 134 yamejengwa, visima 64 vyenye uwezo wa kuzalisha wastani wa lita za maji 177,000,000 kwa saa vimechimbwa pamoja na ulazaji wa mabomba km 466.9.

Kupitia Mradi wa Uimarishaji huduma za maji mijini na vijijini na mradi wa fedha za Ahueni ya UVIKO-19, jumla ya visima 38 vimechimbwa na 28 kati ya hivyo vimeanza kutumika. Serikali pia kipitia ZAWA imefanikiwa kuviendeleza visima 26 kati ya 36 vya Mradi wa maji wa RAK ambavyo vinatoa huduma. Aidha, kazi ya ujenzi wa matangi 10 ya kuhifadhia maji yenye uwezo wa kuhifadhi lita 10,000,000 kwa pamoja umekamilika. Juhudi hizi za Serikali za kuimarisha huduma za maji safi na salama zina lengo la kuhakikisha huduma hii inakuwa endelevu na inawafikia wananchi kwa shehia zote za Unguja na Pemba kwa saa 24.

Ndugu Wananchi,

Ujenzi wa majengo kwa ajili ya makaazi, Ofisi na biashara umepewa umuhimu mkubwa. Serikali imeendeleza ujenzi wa nyumba za makaazi mijini na vijijini. 

Ujenzi wa nyumba za makaazi 276 unaofanywa kupitia Mfuko wa Hifadhi ya Jamii katika eneo la Tomondo umekamilika. Aidha, Serikali kupitia Shirika la Nyumba imekamilisha ujenzi wa nyumba 72 eneo la kwa Mchina na  nyumba 8 na maduka 20 eneo la Mkungumalofa Pemba. Serikali ina lengo la kujenga nyumba 3,000 eneo la Chumbuni ambapo ujenzi wa awamu ya kwanza wa nyumba 1,095 unaendelea. Miradi mingine itakayotekelezwa ni ujenzi wa nyumba 24 Kiembesamaki, nyumba 1095 Kikwajuni, nyumba 548 Kisakasaka B, nyumba 240 Kisakasaka A, nyumba 209 Saateni, nyumba 120 Nyamanzi na nyumba 180 Mabaoni Mfikiwa Pemba. Serikali imetenga maeneo maalum kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za makaazi kwa wananchi kwa kila Wilaya.

Kwa lengo la kuimarisha haiba ya mji na kuondoa changamoto ya kukosa maegesho, Serikali kupitia Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (ZSSF) imekamilisha ujenzi wa maegesho ya kisasa katika eneo la Malindi pamoja na  mradi wa kituo cha mabasi Kijangwani. Jitihada hizi zimekwenda sambamba na ujenzi wa maduka ya biashara na maegesho Darajani, maeneo ya mapumziko na bustani Mnazi mmoja, eneo la mapumziko na michezo ya watoto Mbweni pamoja na eneo la maonesho ya biashara Nyamanzi. Serikali inaendelea kuwakaribisha wawekezaji katika ujenzi wa nyumba za gharama nafuu, kumbi za mikutano na majengo ya biashara.

Ndugu Wananchi,

Kwa kutambua umuhimu wa kilimo, Serikali imefanya juhudi za kuimarisha sekta hiyo. Ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji maji Awamu ya Kwanza katika Mabonde sita (6) yenye ukubwa wa hekta 1,053 katika mabonde ya Kilombero (hekta 292), Cheju A (hekta 315), Kibokwa (hekta 147), Kinyasini Unguja (hekta 184), Chaani (hekta 71) na Mlemele (hekta 44)  yamekamilika. Pia ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji awamu ya pili kati bonde la Cheju B umekamilika ambapo utawanufaisha zaidi ya wakulima 2,100. Lengo la mradi huu ni kuongeza uzalishaji wa mpunga hadi tani 15 kwa hekta  na kuondokana na kilimo cha kutegemea mvua.Serikali imetenga jumla ya TZS bilioni 5.5 kwa ajili ya kuwasaidia wakulima kupata pembejeo za kilimo kwa bei nafuu, zikiwemo mbolea, mbegu, na dawa. 

Ndugu Wananchi,

Tunapoadhimisha miaka 61 ya Mapinduzi mafanikio makubwa yamepatikana katika kuimarisha sekta ya michezo nchini. Serikali imefanya juhudi kubwa kuimarisha miundombinu ya michezo hususani kufanya matengenezo makubwa ya viwanja vya Amani na Gombani viweze kukidhi viwango vya michezo ya kimataifa. Ukarabati wa uwanja wa  Mao Zedong unaendelea pamoja na kuanza ujenzi wa viwanja 17 vya michezo vya Wilaya na Mikoa. Katika kuhakikisha tunaongeza viwanja vya michezo na kwenda sambamba na malengo ya kukaribisha mashindano ya mpira ya CHAN yanayoshirikisha wachezaji wa ndani yanayotarajiwa kufanyika mwezi wa Februari mwaka huu wa 2025 na mashindano ya AFCOM mwaka 2027, Serikali imeanza kuimarisha viwanja vyetu pamoja na kujenga viwanja vipya vya michezo katika maeneo ya Maisara. Aidha, ujenzi wa hoteli ya Amani sambamba na ujenzi wa ukumbi wa Mikutano na maeneo kwa ajili ya michezo ya ndani katika Complex hiyo umekamilika.

Jitihada za kuimarisha miundombinu ya michezo, zimevutia kufanyika kwa mashindano mbali mbali yakiwemo mashindano ya kanda na kimataifa ya mchezo wa wavu, mashindano ya CAF ya African Schools Championship, mashindano ya riadha Afrika Mashariki na Kati na mashindano ya ITF Taekwondo na Martial Arts. Vile vile, baadhi ya timu kubwa kutoka Tanzania bara zimechagua michezo yao kufanyika Zanzibar.

Kwa kuipata hutuba mzima  endelea chini utakutana na Link ya PDF