HOTUBA YA WAZIRI WA NCHI AFISI YA RAIS -IKULU  MHESHIMIWA JAMAL KASSIM ALI

KUHUSU MAKADIRIO YA MATUMIZI YA  FEDHA KWA MWAKA WA FEDHA 2023/2024

 

MEI, 2023

 

YALIYOMO

 

YALIYOMO i

ORODHA YA VIAMBATISHO ii

VIFUPISHO VYA MANENO iv

UTANGULIZI 1

MAFANIKIO YA UTEKELEZAJI WA PROGRAMU ZA AFISI YA RAIS – IKULU KWA MWAKA WA FEDHA 2022/2023 5

MAFANIKIO YA FUNGU A01 5

MAFANIKIO YA FUNGU A02 BARAZA LA MAPINDUZI 44

MWELEKEO WA BAJETI YA AFISI RAIS IKULU KWA MWAKA WA FEDHA 2023/2024 46

PROGRAMU KUU NA NDOGO NA MAKISIO YA FEDHA ZINAZOHITAJIKA KWA MWAKA WA FEDHA 2023/2024       47

PROGRAMU KUBWA NA NDOGO ZA FUNGU A01 49

PROGRAMU KUBWA NA NDOGO ZA FUNGU A02 53

PROGRAMU KUBWA NA NDOGO ZA FUNGU A09 56

PROGRAMU KUBWA NA NDOGO ZA FUNGU A10. 58

MAMBO MAKUU YATAKAYOTEKELEZWA NA AFISI YA RAIS -IKULU KWA MIRADI YA MAENDELEO KWA MWAKA WA FEDHA WA 2023/2024 60

MAOMBI YA FEDHA YA KAZI ZILIZOPANGWA KUTEKELEZWA KWA MWAKA WA FEDHA 2023/2024 61

HITIMISHO 61

 

ORODHA YA VIAMBATISHO

Kiambatisho 1. Mapitio ya Utekelezaji wa Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Bajeti ya mwaka 2023/2024 63

Kiambatisho 2. Malalamiko yaliyowasilishwa na Wananchi kwa Taasisi 59 za Serikali zilizounganishwa katika Mfumo wa Sema na Rais kwa Julai – Machi 2022/2023 70

Kiambatisho 3. Orodha ya Malalamiko yaliyowasilishwa na Wananchi kwa Kipindi cha Miezi 9 Julai - Machi 2022/2023

................................................................................ 74

Kiambatisho 4. Mchanganuo wa Takwimu za Malalamiko kwa Mwezi katika kipindi cha Julai – Machi 2022/2023 kupitia Mfumo wa Sema na Rais 75

Kiambatisho 5. Idadi ya Watumishi Waliopekuliwa kwa Wizara/Taasisi 90

Kiambatisho 6. Idadi ya Watumishi Waliopatiwa Mafunzo kwa Wizara/Taasisi. 93

Kiambatisho 7. Idadi ya Majengo ya Serikali yaliyofanyiwa Ukaguzi wa Kiusalama 94

Kiambatisho 8. Orodha ya Wizara, Idara na Taasisi zilizofanyiwa Ukaguzi kwa kipindi cha Julai-Machi, 2023     96 Kiambatisho 9. Idadi ya Watafiti wa Ndani na kutoka Nje ya Nchi walaiotembelea Taasisi ya Nyaraka na Kumbukumbu kwa kipindi cha Julai-Machi 2023 100

Kiambatisho 10. Wageni wa ndani ya Nchi 101

 

VIFUPISHO VYA MANENO

 

 

AfCFTA

African Continental Free Trade Area (Eneo huru la Biashara Barani Afrika)

AFD

Jumuiya ya Maendeleo ya Ufaransa

CCM

Chama cha Mapinduzi

EAC

East Africa Community (Jumuiya ya Afrika Mashariki)

GCC

Global Cooperation Committee

IORA

Indian Ocean Rim Association (Jumuiya ya Nchi zilizopakana na Bahari ya Hindi

JPC

Joint Permanent Commission (Tume ya kudumu ya Pamoja)

PDB

Presidential Delivery Beaureu

SADC

TADIO                 

Southern African Development Community (Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika)

Tanzania Diaspora in Oman (Jumuiya ya Wanadiapora wa Tanzania Nchini Omani).

UNFPA

Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya watu

UNHIF

Mfuko wa Taifa wa Bima ya afya

WTTC

World Travel and Tourism Council Global Summit

 

ZACADIA

Jumuiya ya Wazanzibari Wanaoishi Nchini Canada (ZACADIA)

ZADEP

Zanzibar Development Plan

ZAWA

Mamlaka ya Maji (Zanzibar Water Authority)

ZBA

Wakala wa Ujenzi Zanzibar

ZBC

Shirika la Utangazaji Zanzibar (Zanzibar Broadcasting Corporation)

ZCTV

Zanzibar Cable Televishion

ZEMA

Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar

ZIPA

Mamlaka ya Ukuzaji Vitega Uchumi Zanzibar

ZPDC

Zanzibar Petroleum Development company

ZPRA

Zanzibar Petroleum Regulatory Authority

 

UTANGULIZI

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwa Baraza lako tukufu kujadili na kuidhinisha makadirio ya mapato na matumizi ya Afisi ya Rais–Ikulu kwa kazi za kawaida na Maendeleo kwa mwaka  wa fedha 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutujaalia mazingira ya amani na utulivu ambayo yametupa nguvu, mshikamano na imani ya kuendelea kumsaidia Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kutekeleza majukumu ya kuongoza Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee napenda kumshukuru Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa imani yake kubwa kwangu kwa kuendelea kuniamini kusimamia Afisi                       ya Rais–Ikulu Zanzibar. Vile vile namshukuru Mheshimiwa Rais kwa safu nzuri ya Watendaji wa Afisi yangu ambao amewaidhinisha.

Mheshimiwa Spika, naomba kuchukua nafasi hii, kumpongeza Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kutimiza miaka miwili (2) na kupata mafanikio makubwa ya utendaji wa kazi yanayoonekana katika sekta mbali mbali nchini. Aidha kipekee nampongeza kwa kuchaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa upande wa Zanzibar. Mheshimiwa Rais wetu amedhihirisha kuwa yeye ni kiongozi bora, muadilifu, mzalendo, mchapa kazi, mpenda mashirikiano na mwenye nia ya kweli katika kuleta  maendeleo nchini.

Mheshimwa Spika, naomba kuchukua nafasi hii kumpongeza Mhe. Dk. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uongozi wake bora, uliojaa uzalendo na maono ambao umechochea kuimarika kwa diplomasia hususani diplomasia ya uchumi baina ya nchi yetu na nchi yengine na mashirika ya kimataifa

Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Othman Masoud Othman  Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar na Mhe Hemed Suleiman Abdallah Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa kuendelea kumsaidia  Mheshimiwa Dk. Hussein Ali Mwinyi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa                             Baraza la Mapinduzi katika kufanikisha majukumu yake ya kuiletea nchi yetu maendeleo.

Mheshimiwa Spika, naomba pia kuwapongeza Mawaziri wenzangu wote wa Serikali ya Awamu ya nane kwa kuendelea kupewa nafasi ya kuwatumikia Wananchi na kutekeleza Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2020 na Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050.

Mheshimiwa Spika, namshukuru Mhandisi Zena Ahmed Said, Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi kwa kazi nzuri anazozifanya katika kutekeleza majukumu yanayoiwezesha Serikali kufikia malengo yake, ikiwa ni pamoja na kuwasimamia Makatibu Wakuu kwa                                    ufanisi.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee naishukuru Kamati ya Kudumu ya kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa ya Baraza la Wawakilishi chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Machano Othman Said, Mwakilishi wa Jimbo la Mfenesini na Makamu wake Mheshimiwa Mtumwa Peya Yussuf, Mwakilishi wa Jimbo la Bumbwini, pamoja na Wajumbe wa Kamati kwa ushirikiano, maelekezo na ushauri mzuri wanao tupatia ambao umetuwezesha kuimarisha utendaji wetu wa kazi.

Mheshimiwa Spika, aidha, naishukuru Kamati ya Bajeti ya Baraza lako tukufu chini ya Mwenyekiti wake Mhe. Abdullah Hussein Kombo Mwakilishi wa Jimbo la Mkoani pamoja na Makamu wake Mhe. Asha Abdallah Mussa Mwakilishi wa   Jimbo la Mahonda pamoja na wajumbe wa kamati kwa michango na miongozo waliotupatia tulipopata bahati ya kuwasilisha Taarifa ya utekelezaji wa Mradi wa Uimarishaji wa Nyumba za Viongozi kwa mwaka 2022/2023 sambamba na kufanya ziara katika maeneo ya mradi.

Mheshimiwa Spika, naomba nikamilishe pongezi zangu kwa namna ya pekee kwako wewe binafsi Mhe. Spika, naibu wako na wenyeviti wa Baraza kwa kuendelea kuliongoza Baraza letu kwa umahiri na mafanikio makubwa. Pili wawakilishi wote kwa kazi nzuri wanazozifanya na ushirikiano wanaonipatia katika utekelezaji wa majukumu ya yangu. Tatu na mwisho napenda kuipongeza na kuishukuru familia yangu  na wapiga kura wa jimbo la Magomeni ambao wameendelea kunipatia upendo, ushirikiano na uvumilivu mkubwa hata pale ninapokuwa nimebanwa na majukumu ya kitaifa nje ya Jimbo langu la uchaguzi. Naahidi kuendelea kushirikiana nanyi katika kuliletea maendeleo jimbo letu na nchi yetu kwa ujumla.

MAFANIKIO YA UTEKELEZAJI WA PROGRAMU ZA AFISI YA RAIS–IKULU KWA MWAKA WA FEDHA 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, Afisi ya Rais-Ikulu, kwa mwaka wa fedha 2022/2023 ilijipangia kutekeleza Programu Kuu sita (06) zenye jumla ya Programu ndogo kumi na tatu (13). Kiambatisho nambari 01 kinamaelezo ya ziada kuhusu Programu Kuu na Programu Ndogo.

MAFANIKIO YA FUNGU A01

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2022/2023, Fungu A01 lilitengewa jumla ya TZS. 15,101.6 Milioni. Kati ya hizo TZS. 6,463.9 Milioni kwa ajili ya Matumizi Mengineo na TZS. 4,637.6 Milioni kwa ajili ya Mishahara na TZS. 4,000.0 Milioni kwa ajili ya Miradi ya Maendeleo. Hadi kufikia                       mwezi Machi, 2023 Fungu A01 liliingiziwa jumla TZS. 1,850.9 Milioni kwa Matumizi Mengineo ambazo ni sawa na asilimia 28.64 na TZS. 470.0 Milioni kwa ajili ya Miradi ya Maendeleo ambazo ni sawa na asilimia 12 ya bajeti iliyopangwa.

Mheshimiwa Spika,  mafanikio ya utekelezaji wa Programu Kuu za Fungu A01 kwa mwaka wa fedha 2022/2023 yako kama ifuatavyo:-

i.Programu Kuu ya Kusimamia na Kuratibu Shughuli na Huduma za Mheshimiwa Rais na Kuimarisha Mawasiliano Ikulu.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2022/2023, Programu hii iliidhinishiwa jumla ya TZS. 5,908.4 Milioni. Kati ya hizo TZS. 2,908.8 Milioni kwa ajili ya Matumizi Mengineo na TZS.2,999.5 Milioni kwa ajili ya Mishahara.                                     Hadi kufikia mwezi Machi, 2023 programu hii iliingiziwa jumla ya TZS. 973.4 Milioni sawa na asilimia 33.46 kwa ajili ya Matumizi mengineo. Utekelezaji wa Programu ndogo katika Program kuu hii ni kama ifuatavyo:-

a.Programu Ndogo ya Kusimamia Huduma na Kuratibu  Shughuli za Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, kwa Mwaka wa Fedha 2022/23, kupitia Programu Ndogo ya Kusimamia Huduma na Kuratibu Shughuli za Mheshimiwa Rais Afisi ya Rais-Ikulu imepata mafanikio yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, naomba kukuarifu kuwa utekelezaji wa Programu hii, umewawezesha watumishi wa Afisi ya Rais- Ikulu Zanzibar kufanikiwa kutoa ushauri kwa Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katika masuala ya Siasa, Uchumi, Jamii, Sheria, Diplomasia, Mawasiliano na Habari, Uhusiano wa Kikanda, Kimataifa na ushauri mwingine kwa lengo la kumsaidia Mheshimiwa Rais kufanya maamuzi sahihi. Aidha, ratiba za matukio ya kila siku zimeendelea kuandaliwa na kufuatwa kulingana na miongozo anayoitoa. Vile vile Afisi imefanikisha kwa ukamilifu jukumu la  msingi la kumpatia huduma anazozihitaji Mheshimiwa Rais pamoja na familia yake.

Mheshimiwa Spika, kupitia utaratibu wa kupokea na kuwakirimu wageni wa ndani na nje ya nchi wanaofika Ikulu kuonana na kuzungumza na Mheshimiwa Rais. Afisi imefanikiwa kuimarisha mahusiano mazuri na nchi marafiki, mashirika ya kimataifa pamoja na wadau wengine wa maendeleo nchini. Kwa kipindi cha miezi tisa ya utekelezaji wa Programu hii, jumla ya wageni elfu moja mia sita na arubaini na tano (1,645) wa ndani na mia saba na hamsini (750) wa nje ya nchi waliweza kufika na kuonana na kuzungumza na Mhe. Rais kwa shughuli mbali mbali za kiserikali na kibinafsi. Aidha, Mhe. Rais katika kipindi hiki alikutana na Mabalozi na viongozi kutoka Mataifa mbali mbali na Jumuiya za Kimataifa waliofika Ikulu. Miongoni mwao ni Rais wa Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo Mhe. Felex Tshisekedi, Balozi wa Japan Mhe. Misawa Yasushi, Balozi wa Kenya Mhe. Isaac Njenga.   Wengine ni Balozi wa Sweden Mhe. Charlotta Ozaki Macias, Balozi wa Afrika Kusini Mhe. Noluthando Mayende Mapele na Balozi mdogo wa U.A.E Mhe. Saleh Ahmed Alhemeir.

Mheshimiwa spika, katika kipindi hiki Mhe. Rais ameweza kuonana na Wawekezaji wa Makampuni kutoka Mataifa mbali mbali duniani. Miongoni mwa Wawekezaji hao ni kutoka Korea, Kampuni ya Global Cooperation Committee (GCC) wakiongozwa na Mwenyekiti wao na Wawekezaji kutoka Uingereza na Uturuki ambao wote  wameonesha nia ya kutaka kuwekeza Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, kwa nia ya kukuza na kuendeleza Diplomasia ya uchumi (Economic Diplomacy) kwa maslahi ya nchi na wananchi kwa ujumla. Afisi imefanikiwa kuratibu na kusimamia ziara mbili (02) nje ya nchi. Moja nchini Oman aliyoifanya mwezi Oktoba 2022. Kupitia ziara hii, Mhe. Rais amepata fursa ya kuwaelezea hali ya utulivu ilivyo Zanzibar na kuwaomba kuja kwa lengo la kuekeza. Ametumia ziara hiyo kuelezea vivutio vya uwekezaji vilivyopo Zanzibar kwa wafanya biashara wa Oman.

Mheshimiwa Spika, mambo muhimu yaliyohusishwa katika majadiliano kati ya Zanzibar na Oman ni pamoja na ushirikiano wa eneo la elimu, ujenzi wa kituo cha data, Uhifadhi wa nyaraka za historia na ukusanyaji wa ushuru kupitia mfumo wa mtandao. Aidha, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilitiliana saini na Serikali ya Omani juu ya Mashirikiano (MOU) kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la Beit–El-ajaib lililopo Forodhani Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, ziara nyengine ni ya Riyadh nchini Saudi  Arabia, ambayo Mhe. Rais Mwinyi alimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk. Samia Suluhu Hassan katika Kongamano la Kimataifa la World Travel and Tourism Council Global Summit (WTTC) lililojadili mustakabali mzima wa sekta ya Utalii.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa ziara za ndani ya nchi, Afisi imefanikiwa kuratibu na kusimamia ziara ya Mhe. Rais katika Wilaya zote za Unguja na Pemba zilizofanyika kati ya tarehe 16 Julai hadi tarehe 28 Julai, 2022. Kupitia ziara hizo,Mhe. Rais alikagua na kuweka mawe ya msingi miradi 54 ya maendeleo ikiwemo ya Serikali 44 na ile ya Binafsi 10. Miongoni mwa miradi hiyo ni ile ya Ujenzi wa Skuli kwa  Unguja na Pemba. Aidha, miradi mingine ni Mabanda ya Wajasiriamali Chumbuni na Pale Kiongele, ukaguzi wa mradi wa Hospitali ya Mkoa ya Lumumba na Hospitali ya Panga tupu. Kwa upande wa sekta binafsi Miradi iliyotembelewa na kuwekwa mawe ya msingi ni  viwanja vya michezo vya Kisakasaka, Skuli ya Combrige Nyamanzi na Hoteli ya Palolo Matemwe.

Mheshimiwa spika, ziara hizi pia zilihusisha ufunguzi wa hoteli yenye hadhi ya nyota tano ya Riu Jambo iliyopo Wilaya ya Kaskazini ‘A’, ufunguzi wa Tawi la CRDB Bank Wete Pemba, Mradi wa Umwagiliaji maji Kinyasini, Ukaguzi na ufunguzi wa miradi ya maji katika maeneo ya mjini na vijijini pamoja na kuweka mawe ya msingi katika miundombinu ya barabara. Sambamba na yote hayo, Mhe. Rais alitumia ziara hizi kusikiliza kero za wananchi zikiwemo za migogoro ya ardhi.

Mheshimiwa spika, ziara hii imeweza kuleta mafanikio makubwa sana kwa kutatua changamoto mbali mbali zilizokua                                       zinawakabili wananchi zikiwemo zile za huduma ya maji safi, miundombinu, umeme, afya na masuala ya ardhi.

Mheshimiwa Spika, Afisi imefanikiwa kufuatilia kwa ukaribu utekelezaji wa ahadi na maagizo ya Mheshimiwa Rais katika sekta mbali mbali nchini. Jumla ya ahadi thalathini na nne (34) zimeweza kutekelezwa. Miongoni mwa ahadi hizo ni pamoja na kuwapatia wananchi wa maeneo mbali mbali ya Unguja na Pemba boti za uvuvi za kisasa 107 (Unguja boti 30 na Pemba boti 77), kuwapatia kompyuta mpakato “laptop” 1,000 wanafunzi wa Kidato cha nne na cha sita waliofaulu vizuri. Ahadi nyengine zilizotekelezwa ni kufanya matengenezo ya Msikiti wa Forodhani, kushughulikia maslahi ya wafanyakazi wa kawaida wa Tume ya Maadili ya Viongozi Zanzibar ili walingane na taasisi zenye majukumu yanayofanana na taasisi yao pamoja na kuipatia tume hiyo watumishi wanne wa kada ya sheria ili kukidhi mahitaji.