RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mheshimiwa Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza azma ya Zanzibar kukuza na kuimarisha uhusiano kati yake na Morocco hasa katika masuala ya kiuchumi, kijamii na kiutamaduni kwa faida ya nchi mbili hizo pamoja na watu wake

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika mazungumzo kati yake na Balozi wa Ufalme wa Morocco katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Abdelilah Benryane, mazungumzo yaliofanyika Ikulu mjini Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alimuhakikishia Balozi Benryane kuwa Zanzibar itaimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano kati yake na Morocco huku akieleza kuwa Zanzibar ina mambo mengi ya kujifunza kutoka nchini humo.

Dk. Shein alisema kuwa ziara ya kiongozi wa nchi hiyo Mfalme Mohammed VI aliyoifanya hapa nchini mnamo mwezi Oktoba mwaka jana imeonesha dalili za uhusiano na ushirikiano mwema kati ya Tanzania na Morocco.

Aliongeza kuwa katika ziara hiyo muhimu ambapo Tanzania ilisaini makubaliano takriban 24 ya ushirikiano kati yake na Morocco katika sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo kilimo, gesi, mafuta, utalii na nyenginezo.

Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa kutokana na Zanzibar kuwa ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, makubaliano hayo pia, yataifaidisha Zanzibar kwa upande wake na kusisitiza kuwa kutokana na hatua hiyo kuna umuhimu mkubwa wa kuzidisha mashirikiano ili makubaliano hayo yaweze kwenda vizuri zaidi.

Aidha, Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya utalii na kusisitiza haja ya kuwepo kwa mashirikiano hasa ikizingatiwa Morocco ni miongoni mwa nchi za Bara la Afrika iliyopiga hatua kubwa katika sekta ya utalii.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo umhimu wa kushirikiana katika sekta nyenginezo ambazo nchi hiyo imepiga hatua ikiwa ni pamoja na sekta ya afya, elimu na utamaduni huku akimueleza haja kwa pande mbili hizo kuanzisha proramu za wanafunzi kutembeleana kimasomo kwa ajili ya kujenga utaalamu na uzoefu.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji wa Morocco kuja kuekeza Zanzibar katika sekta mbali mbali ikiwemo sekta ya uvuvi hasa wa bahari kuu na kumueleza balozi huyo wa Morocco haja ya kuitangaza Zanzibar nchini mwake kiutalii.

Aliongeza kuwa Zanzibar ina sifa zote za uwekezaji hasa katika sekta hiyo ya uvuvi hasa ikizingatiwa kuwa ni nchi ya visiwa vilivyozungukwa na bahari ambayo ina samaki wengi ambao ni maarufu na wanaopendwa duniani wakiwemo samaki aina ya jodari.

Nae Balozi wa Ufalme wa Morocco katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Abdelilah Benryane alimueleza Dk. Shein kuwa Morocco inajivunia uhusiano na ushirikiano mwema uliopo kati yake na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar.

Balozi Benryane alisema kuwa Morocco iko tayari kushirikiana na Zanzibar katika kuendeleza miradi mbali mbali ya maendeleo na kumuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa nchi yake itatoa nafasi za masomo katika kada mbali mbali kwa wanafunzi wa elimu ya juu wa Zanzibar ikiwa ni pamoja na nafasi za masomo ya elimu ya dini.

Aidha, alieleza haja ya kuwepo mashirikiano ya kubadilishana uzoefu na utaalamu kwa wanafunzi wa Zanzibar na wale wa nchi yake kutokana na nchi hiyo kuwa na vyuo vingi vinavyotoa mafunzo kadhaa.

Pamoja na hayo, Balozi huyo alimuhakikishia Dk. Shein kuwa juhudi za makusudi atazichukua katika kuhakikisha anajenga mashirikiano mazuri nchini mwake kwa kuendeleza uhusiano na ushirikiano na Zanzibar katika sekta muhimu za maendeleo zikiwemo elimu, afya, kilimo, uvuvi, utalii na nyenginezo 

Akizungumzia juu ya sekta ya utalii, Balozi huyo alisema kuwa nchi yake imepiga hatua kubwa katika sekta hiyo ambapo hivi sasa inapokea watalii milioni 16 kwa mwaka kufuatia program ijulikanayo ‘Azur Blue’ iliyoanzishwa na kiongozi wa nchi hiyo Mfalme Momamed VI ambapo pia, katika programu ya pili wamejiwekea hadi kufikia mwaka 2020 watapokea watalii wapatao milioni 20.

Hivyo, alieleza kuwa nchi yake itakuza uhusiano na Zanzibar katika kuimarisha sekta hiyo hasa ikizingatiwa kuwa nchini mwake kuna miundombinu mingi ya kuimarisha sekta hiyo vikiwemo vyuo vya mafunzo ya kitalii.