Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na UN Women katika kukuza usawa wa kijinsia, kuwawezesha wanawake kiuchumi na kuzuia ukatili dhidi ya wanawake na wasichana.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 22 Julai 2026, Ikulu Zanzibar, alipokutana na Mwakilishi mpya wa UN Women nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard, aliyefika kujitambulisha rasmi baada ya kuanza majukumu yake.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza kuimarishwa kwa ushirikiano katika maendeleo ya sekta ya mwani, matumizi ya takwimu za kijinsia, bajeti zinazozingatia usawa wa kijinsia na kuongeza ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi.

Kwa upande wake, Bi. Julia Broussard ameipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa hatua zinazochukua katika kukuza usawa wa kijinsia na kuahidi kuwa UN Women itaendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali katika kuwawezesha wanawake na kuboresha ustawi wa wanawake na wasichana Zanzibar.