Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amejumuika na wanafamilia, viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na wananchi mbalimbali katika dua maalum ya kumuombea aliyekuwa Rais wa Awamu ya Pili wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Mzee Ali Hassan Mwinyi.
Dua hiyo imefanyika leo, tarehe 05 Aprili 2026, katika Msikiti wa Ali Hassan Mwinyi uliopo Mangapwani, Mkoa wa Kaskazini Unguja, ikiwa ni utaratibu maalum wa kuwaombea waasisi na viongozi wa Taifa waliotangulia mbele ya haki, kuelekea maadhimisho ya kumbukumbu ya Rais wa Kwanza wa Zanzibar, Hayati Sheikh Abeid Amani Karume, yatakayofanyika tarehe 07 Aprili 2026.
Dua hiyo maalum imeandaliwa na Wizara ya Nchi, Afisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ kushirikiana na Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar.
Akizungumza katika dua hiyo, Waziri wa Nchi, Afisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ, Mhe. Idrissa Kitwana Mustafa, amesema Serikali itaendelea kumuenzi Hayati Mzee Ali Hassan Mwinyi kwa mambo makubwa na mazuri aliyoifanyia nchi yake wakati wa uhai wake.
Aidha, amempongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa kuendeleza utaratibu huo wa kuwaenzi, kuwaombea na kuwakumbuka waasisi na viongozi wa Taifa waliotangulia mbele ya haki.
