Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesisitiza umuhimu wa kuendelea kulinda na kudumisha amani, umoja na mshikamano nchini, akihimiza wananchi kuondoa ubaguzi na kuimarisha upendo katika jamii. Amesema umoja wa wananchi ni msingi muhimu wa utulivu wa Taifa, na kila mmoja ana wajibu wa kulinda tunu hizo kwa vitendo.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, Aprili 03, 2026, baada ya kushiriki Sala ya Ijumaa iliyoambatana na Dua Maalum ya kuiombea nchi, viongozi na marehemu, iliyofanyika Msikiti wa Mzee Ali Hassan Mwinyi, Mangapwani.Dua hiyo imeandaliwa na Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar kwa kushirikiana na Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Juma Malik Akil, na imefanyika katika Msikiti wa Mzee Ali Hassan Mwinyi uliopo Mangapwani, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Aidha, amewataka waumini kuepuka makundi yenye viashiria vya chuki na migawanyiko, akisisitiza kuwa dini inahimiza amani na uvumilivu. Dua hiyo imehudhuriwa na Mke wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Mama Mariam Mwinyi, viongozi mbalimbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, viongozi wa dini pamoja na ndugu, jamaa na marafiki.

Sambamba na hayo, Rais Dkt.Mwinyi, akiwa ameambatana na viongozi mbalimbali wa Serikali na waumini, walizuru kaburi la Hayati Mzee Ali Hassan Mwinyi kwa ajili ya kumuombea dua maalum.