RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi ameihakikishia Serikali ya Saudi Arabia ushirikiano mzuri uliopo na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hasa kwenye miradi mbalimbali ya Maendeleo.

Rais Dk. Mwinyi ameyasema hayo Ikulu Zanzibar, alipozungumza na Balozi wa Saudi Arabia nchini Tanzania, Mhe. Yahya Ahmad Okeish na ujumbe wake kwa lengo la kuimarisha ushirikiano uliopo baina ya nchi mbili hizo.Dk. Mwinyi alisema, SMZ ni mnufaika mkubwa wa mfuko wa Saudia na Quwait kwenye miradi yake ya maeneleo kupitia ushirikiano mzuri uliopo baina ya mataifa hayo.

Aidha, Rais Dk. Mwinyi ameishukuru na kuipongeza Serikali ya Saudi Arabia kwa ushirikiano wake na Tanzania hususan kuipatia Zanzibar zawadi mbalimbali inazozituma kwa watu wa Zanzibar ikiwemo tende wakati wa Mwezi mtukufu wa Ramadhan.

Katika salamu zake kwa Tanzania, Balozi Okeish amepongeza mafanikio makubwa yaliyofikiwa na taifa hili kwa kutimiza miaka 60 ya Muungano wake baina ya Tanganyika na Zanzibar sambamba na kuuombea mafanikio zaidi muungano huo.
Pia, Balozi Okeish alisifu ushirikiano wa diplomasia uliopo baina ya Saudi Arabia na Tanzania ikiwemo Zanzibar pamoja na kusifu tamaduni za pande mbili hizo.