Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuwa uwasilishaji wa Tamko la Pamoja baina ya Chama Cha Mapinduzi na ACT Wazalendo ni hatua muhimu inayofungua njia ya utekelezaji wa uundaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa, pamoja na kuimarisha amani, umoja, mshikamano na mustakabali mwema wa Zanzibar. Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 09 Julai 2026, baada ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja na utiaji saini wa Agenda za Kuchukuliwa Hatua baina ya Chama Cha Mapinduzi na ACT Wazalendo, hafla iliyofanyika katika Viwanja vya Ikulu, Zanzibar.
Amesema hatua hiyo ni kielelezo cha dhamira ya dhati ya viongozi wa Zanzibar kuendeleza mazungumzo, kujenga kuaminiana na kuweka mbele maslahi mapana ya nchi na wananchi wake, ikiwa ni msingi muhimu wa kuimarisha utulivu wa kisiasa, mshikamano wa kijamii na maendeleo endelevu.Ra is Dkt. Mwinyi amewahakikishia viongozi wa vyama vya siasa na wananchi wa Zanzibar kuwa yuko tayari kushirikiana na viongozi wenzake kuyaendeleza kwa dhati maridhiano hayo, kwa lengo la kuhakikisha Zanzibar inaendelea kuwa na amani, umoja, mshikamano na utulivu.
Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesema katika utekelezaji wa awamu inayofuata ya maridhiano hayo, maslahi mapana ya nchi yataendelea kupewa kipaumbele, hatua itakayosaidia kuimarisha imani ya wananchi, wadau na washirika wa maendeleo katika mwelekeo wa kisiasa, kijamii na kiuchumi Zanzibar. Amesisitiza kuwa mchakato huo haupaswi kuangaliwa kama suala la kisiasa pekee, bali ni hatua yenye umuhimu mkubwa katika kujenga misingi imara ya utawala bora, uwajibikaji, utoaji haki, utengamano wa kijamii na maendeleo ya muda mrefu kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.
Rais Dkt. Mwinyi amesema Zanzibar inahitaji kuendelea kuimarisha misingi ya kuaminiana, kuvumiliana, kuheshimiana na kushirikiana, kwa kuwa mambo hayo ni nguzo muhimu katika kulinda amani, kukuza maendeleo na kuiwezesha Zanzibar kufikia malengo yake ya muda mrefu. Rais Dkt. Mwinyi ametoa wito kwa viongozi wa vyama vya siasa, viongozi wa dini, wananchi na wadau wote kuunga mkono dhamira hiyo njema, kwa kuendeleza moyo wa mazungumzo na kuweka mbele maslahi ya Zanzibar kuliko maslahi binafsi au ya kisiasa.
Amesema wananchi wengi wanaunga mkono maridhiano hayo, hivyo ni wajibu wa viongozi wote kuendelea kuwafahamisha wananchi umuhimu wa mchakato huo katika kuimarisha demokrasia, amani, haki, umoja, mshikamano na maendeleo. Dkt. Mwinyi pia amewataka viongozi wa dini kutoa baraka zao na kuyaombea dua maridhiano hayo, akieleza kuwa yana umuhimu mkubwa kwa maslahi ya wananchi wa Zanzibar na maendeleo ya nchi kwa ujumla.
Mapema, Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, ambaye pia ni Katibu wa Kamati ya Maridhiano, aliwasilisha Tamko la Pamoja lililobeba vipengele muhimu. Uwasilishaji huo ulifuatiwa na tukio la utiaji saini wa Ajenda za Kuchukuliwa Hatua, ambapo Chama Cha Mapinduzi kiliwakilishwa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Dkt. Mohamed Said Dimwa, huku ACT-Wazalendo ikiwakilishwa na Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, Ndg. Omar Ali Shehe.
Akitoa nasaha zake, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepongeza hatua hiyo na kueleza kuwa maridhiano yaliyofikiwa yanafungua ukurasa mpya wa kuimarisha umoja, utulivu na mshikamano miongoni mwa Wazanzibari. Aidha, amesema hatua hiyo ni ishara ya ukomavu wa kisiasa na uthibitisho wa dhamira ya viongozi pamoja na wadau wa siasa katika kujenga mazingira ya amani, ushirikiano na maendeleo endelevu kwa Zanzibar na Taifa kwa ujumla.
Naye, Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo Taifa, Mhe. Othman Masoud Othman, amempongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa hatua alizochukua katika kuendeleza mchakato huo, ambao umefungua njia ya kupatikana kwa ufumbuzi wa kudumu wa changamoto za kisiasa Zanzibar. Tukio hilo pia limehudhuriwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi; Marais Wastaafu wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume na Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein; Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla; viongozi wa vyama vya siasa, viongozi wa dini, viongozi wa Serikali SMT na SMZ, Mabalozi wanaoziwakilisha nchi za Tanzania, Taasisi mbalimbali za Kimataifa na wananchi.