Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema dhamira ya viongozi kufikia maridhiano katika ngazi ya kitaifa ni kuwaunganisha wananchi, kuimarisha umoja wao na kuwawezesha kushirikiana katika kuleta maendeleo ya nchi.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 10 Julai 2026, alipojumuika na waumini wa dini ya Kiislamu katika Sala ya Ijumaa na ufunguzi wa Msikiti wa Abrar, uliopo Fuoni Kibondeni, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Amesema ili kufikia malengo hayo, wananchi wanapaswa kusahau yaliyopita, kusameheana, kuachana kabisa na mifarakano iliyokuwepo na kusonga mbele kwa pamoja kwa ajili ya maendeleo katika nyanja mbalimbali.

Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza kuwa umoja, mshikamano, amani na maelewano ndani ya jamii ni misingi muhimu inayoiwezesha Serikali kupanga na kutekeleza miradi pamoja na mipango mbalimbali ya maendeleo. Hivyo, amewahimiza wananchi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuwaletea maendeleo.

Akizungumzia ufunguzi wa msikiti huo, Rais Dkt. Mwinyi amewahimiza waumini wa dini ya Kiislamu kuitumia misikiti kama sehemu ya ibada, malezi na majadiliano kuhusu changamoto zinazoikabili jamii, ili kuzipatia ufumbuzi wa kudumu. Amezitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni matumizi ya dawa za kulevya, wizi, uporaji, ujambazi na vitendo vya rushwa miongoni mwa watumishi wa umma.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi ametoa wito kwa jamii kuendelea kuwasaidia mayatima, wajane, watu wenye ulemavu na makundi mengine yenye mahitaji maalumu.

Vilevile, amewahimiza waumini kuweka mkazo katika kuwapatia vijana elimu ya dini na malezi yanayozingatia maadili mema, ili kujenga kizazi chenye hofu ya Mwenyezi Mungu na chenye uwezo wa kuwa raia wema na wenye manufaa kwa nchi yao.

Akihitimisha hotuba yake, Rais Dkt. Mwinyi ameipongeza Taasisi ya Al Hilal Islamic Center kwa kujenga msikiti huo na kuwanasihi waumini kuutunza na kudumisha usafi wake wakati wote, ili uwe na mazingira bora ya kufanyia ibada.
Pia, amewashauri waumini kuweka utaratibu maalumu wa kuwasaidia maimamu, walimu wa madrasa na watu wengine wanaohudumia misikiti, ili waweze kukidhi mahitaji yao ya kila siku kutokana na muda mwingi wanaoutumia katika kuwahudumia waumini na kusimamia shughuli za misikiti.

Wakati huohuo, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amemtembelea na kumjulia hali Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Magharibi Kichama, Ndg. Muhammed Rajab Soud, aliyelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mjini Magharibi, Lumumba.