RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein ameutaka uongozi wa Shirika la utangazaji Zanzibar (ZBC) kuwa na mipango madhubuti ya kuwapatia mafunzo wafanyakazi wake ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi.
Dk.Shein amesema hayo wakati alipokuwa akitoa ufafanuzi kwa Viongozi na wafanyakazi wa Shirika hilo (ZBC Redio) juu ya hoja mbali mbali zilizoibuliwa katika mkutano uliofanyika ukumbi wa Idara ya Utamaduni Rahaleo, Mjini hapa.
Alisema kuna umuhimu mkubwa kwa uongozi wa shirika hilo kuwa na mipango madhubuti ya muda mfupi na mrefu, itakayowawezesha wafanyakazi hao kupata mafunzo ndani na nje ya nchi, na hivyo kuliwezesha shirika hilo kupata wataalamu wanaohitajika katika kuliendeleza.
Alisema ni jambo jema kwa uongozi huo ukandaa mipango hiyo kuambatana na vitengo vilivyopo na kuwapatia fursa hizo wafanyakazi bila ya maombi au kufanya upendeleo wowowte.
Aidha, alitaka kuwepo uwiano kati ya Uongozi wa Shirika hilo, Wizara na Bodi ya Shirika katika kuzitafutia ufumbuzi changamoto mbali mbali zinazojitokeza, akibainisha kuwepo mapungufu katika kushughulia masuala hayo hivi sasa.
Vile vile alitaka kufanyika juhudi katika upatikanaji wa nyenzo, ikiwemo fedha za kujikimu, usafiri na vifaa ili kufanikisha kazi pale waandishi wanapotoka nje ya vituo vyao vya kazi kwa ajili kutafuta habari.
Rais Dk. Shein alisema Wizara kwa mashirikiano na taasisi zake inapaswa kuwa na vipaumbele vya mahitaji kutoka katika vitengo vyake vyote na hivyo kutatuwa changamoto zolizopo kwa mujibu wa bajeti ya fedha zitakazopatikana.
Vile vile Dk. Shein alitowa rai kwa uongozi wa Wizara na ZBC kuwaruhusu bila vikwazo wafanyakazi wote wanaohitaji uhamisho wa kwenda taasisi nyeingine ya Serikali, pale panapokuwa na makubaliano kati ya Taaasisi moja na nyingine.
Katika hali hiyo, Dk. Shein alisema ni jambo jema kwa Viongozi hao kuwajengea mazingira bora na kuvutia wafanyakazi wao ili waendelee kubaki katika maeneo yao ya kazi, na kuainisha kuwa pale wanapotoka kuondoka, basi ni vyema wakaruhusiwa bila vikwazo.
Katika hatua nyengine, Dk. Shein alisema ZBC ni Shirika jipya la Serikali lililoundwa kwa lengo la kuimarisha huduma za Utangazaji nchini ili kuchochea maendeleo.
Alisema Bodi ya ZBC ina jukumu kubwa la kusimamia na kuliongoza Shirika hilo ili kufikia mafanikio yaliolengwa.
Alisema madhumuni makubwa ya serikali kuziunganisha taasisi za Redio na Televisheni umezingatia wafanyakazi wote wa vyombo hivyo kuwa wamoja na wenye maingiliano ya karibu katika utendaji wa kazi zao.
Alisema Shirika hilo lina malengo yalio sawa na mashirika mengine ya Kimataifa kama vile DW, BBC, Aljazeera na mengineyo, yakitofautiana na ZBC kutokana na uwezo wake wa kiutendaji.
Alieleza kuwa Shirika hilo lina kazi kubwa ya kufanya mbele yake ili kufanikisha malengo yaliokusudiwa pamoja na kushinda vikwazo mbali mbali vinavyozorotesha maendeleo.
“Kazi ya kulifanya Shirika hilo kupata mafanikio sio ya kufumba na kufumbua, bali inahitaji muda mwingi2, alisema.
Alisema Serikali imegharamika sana katika uundaji wa Shirika hilo kwa kutumia zaidi ya shilingi Bilioni 17 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa na mitambo, hivyo akasistiza umuhimu wa ZBC, Bodi na Wizara kushirikiana, sambamba na kuitaka Bodi kufanyakazi ya kuwatumikia na kuwaunganisha wafanyakazi,pamoja na kuwashajiisha kufanya kazi zao kwa bidii.
“……..hayo mashirika makubwa , nayo yamepita katika hali hii hii kwa taabu, kujenga ni kazi kubwa na mimi ninavyoliona shirika hili litafanikiwa sana”, alisema.
Alisema hivi sasa Shirika hilo bado linategemea ruzuku kutoka serikalini katika upatikanaji wa mahitaji mbali mbali kwa ajili ya wafanyakazi wake, ikiwa pamoja na vifaa.
Akigusia historia ya Utangazaji Zanzibar, Dk. Shein alisema Zanzibar ina mengi ya kujivunia, akibainisha kuwepo wafanyakazi wengi kutoka nchi mbali mbali za Afrika Mashariki na Duniani kwa ujumla waliokuja nchini kujifunza.
Mapema, Katibu Mkuu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Dk. Abdulahamid Yahya Mzee, akitoa ufafanuzi wa masuala mbali mbali alisema, Serikali inatowa kipaumbele kwa jamii ya watu wenye ulemavu pale zinapotokea fursa za ajira na kuwepo watu wengine wenye sifa zinazofanana.
Aliwataka watu wenye ulemavu kuwasilisha malalamiko yao serikalini pale wanapobaini taratibu za ajira kuvunjwa, pamoja na kuwataka waajiri kuisaidia ajmii hiyo kutokana na hali zao.
Alisema Serikali imekuwa ikiwashajiisha wafanyakazi kusoma na kuwataka kuondokana na utamaduni wa kukimbilia vyuo vya nje katika aina ya masomo ambayo vyuo vya ndani vinafundisha.
Alisema Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma, imeamuwa kuwa an mfuko wa kuwaendeleza kitaaluma watumishi wa serikali, sambamba na kuzitaka taasisi zote kutenga fedha kwa ajili ya kusomesha wafanyakazi wao.
Akigusia suala la uhamisho wa wafanyakazi kutoka taasisi moja kwenda nyingine, Dk. Abdulahamid alisema kinachohitajika ni makubaliqno kati ya taasisi mbili na kubainisha pale panapokosekana makubaliano, Katibu Mkuu Kiongozi ndie mwenye dhima ya kutoa maamuzi kwa maslahi ya Taifa.
Aidha, alitoa ufafanuzi juu ya Posho la mazingira magumu na kusema kuwa kila mfanyakazi anapaswa kutambua aina ya kazi na changamoto zake pale anapoajiriwa.
Alisema Serikali tayari imetowa madaraja kwa kila shirika, hivyo kila mfanyakazi wa shirika linalohusika atapaswa kupata posho kulingana na aina ya daraja la shirika analofanyia kazi.
Nae, Waziri wa Habari, Utamaduni na Mambo ya kale, Mahamoud Thabit kombo, aliwataka Viongozi wa Vitengo vilivyomo ZBC kukaa pamoja na kuyatafutia ufumbuzi matatizo yanayojitokeza na pale inaposhindikana kuyatuma uongozi wa juu kwa hatua.
Alisema uongozi wa Wizara hiyo utaendelea kusimamia vikao vya ngazi za chini za uongozi ili kutatuwa matatizo mbali mbali yaliojitokeza ikiwemo uchakavu wa majengo na mahitaji ya vifaa mbali mbali vyenye gharama nafuu.
Akizungumzaia suala la mafunzo kwa wafanyakazi, alisema hatua zinaendelea kuchukuliwa , kukiwa na matarajio makubwa ya kupatikana fursa hizo pamoja na kuongeza idadi ya mafundi kupitia vijana wapya watakaosomeshwa kwa kuzingatia wale wachache waliopo wako njiani kustaafu.
Vile vile, Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni na Mambo ya Kale, Khadija Bakari alitowa wito kwa wafanyakazi kutekeleza majukumu yao kuambatana na maadili, silka, kanuni na miongozo ya Utumishi wa Umma.
Wakati huo huo, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alikutana na Uongozi na wafanyakazi wa Shirika la Magazeti ya Serikali.
Akitoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizoibuliwa na wafanyakazi wa Shirika hilo, Dk. Shein alitaka kuwepo mashirikiano ya pamoja baina ya Menejment ya Shirika, Bodi, Wizara na Serikali Kuu ili kufikia mafanikio na kutaka kila mmoja ana dhima ya kutekeleza wajibu wake.
Alisema lengo na mipango ya Serikali ni kuwa na Shirika lenye nguvu na linalojitegema wenyewe, litakaloweza kulipa mishahara, maposho, mahitaji ay usafiri an kutoa huduma nyingine mbalimbali.
Alisema mahitaji ya wafanyakazi na mengineyo yatapaswa kuidhinishwa na Bodi ya Shirika hilo, sambamba na kuwashajiisha wafanyakazi kupenda kusoma, kwa kigezo kuwa Shirika linahitaji watu wenye taaluma ya kutosha.
Aidha, aliwapongeza wafanyakazi wa Shirika hilo kwa kazi nzuri ya kuendeleza gazeti hilo.
Alisisitiza umuhimu wa wafanyakazi kujikita katika kutafuta taaluma, kwa kigezo kuwa ndio msingi wa maendeleo yoyote Duniani.
Nae, Katibu Mkuu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulahamid Yahya Mzeee, aliutaka uongozi wa Shirika hilo kufanya mambo yake kwa uwazi, hususan katika suala la maslahi ya wafanyakazi (posho) na kufuata taratibu ili kuondoa manung’uniko miongoni mwa wafanyakazi.
Kuhusiana na suala la masomo, Dk. Mzee alisisitiza haja ya kuwepo programu maalum ya mafunzo kwa wafanyakazi, ili taasisi iweze kukidhi mahitaji yake ipasavyo.
Alisema kwa yale masomo yalio katika kada maalum, ambapo mafunzo yake hupatikana nje ya nchi, ameelekeza mapendekezo ya namna hiyo yatumwe Serikali ili yaweze kuchukuliwa hatua.
Waziri wa Habari, Utalii na Mambo ya Kale Mahamoud Thabit Kombo alisema uwepo wa makundi na matabaka miongoni mwa watendaji wa shirika hilo ni jambo linalodumaza maendeleo ya shirika.
Alisema uongozi wa Wizara hiyo umejipanga kulishughulikia suala hilo ili ufumbuzi wa kudumu uweze kupatikana na kurudisha mshikamano kazini.
Aidha, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Magazeti ya serikali Yussuf Khamis alitowa pongezi kwa serikali kwa kulipatia makazi bora Shirika hilo, hivyo kuwa katika mazingira bora zaidi ya kiutendaji.
Alisema wakati Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein akitimiza miaka tisa ya uongozi wake, Shirika hilo linajivunia kuanzisha gazeti jipya la ‘Zanzibar Mail’ linalochapishwa kwa lugha ya Kiingereza.
Katika mikutano hiyo wafanyakazi wa mashirika hayo mawili walipata fursa ya kuibuwa hoja katika nyanja mbali mbali, ikiwemo upatikanaji wa fursa za masomo, matatizo ya usafiri, ajira, usalama, posho la usumbufu na nyenginezo.