RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi ameendelea kusisitiza dhamira yake njema ya kuiunganisha tena Zanzibar kuwa moja yenye amani, upendo, maridhiano na mshikamo.Ameyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozindua tena Kamati ya Maridhiano baina ya Chama cha Mapinduzi na ACT Wazalendo ifanyekazi pamoja kuendeleza amani iliyopo nchini.

Alisema bado ana nia ya kuiendeleza Zanzibar kuwa moja bila kujali rangi, asili, imani za dini, au itikadi za kisiasa kama alivyoahidi kwa mara ya kwanza alipohutubia Baraza la Wawakilishi mwezi Novemba, 2022 juu ya dhamira yake ya kuwaunganisha wananchi wa Zanzibar kuwa wamoja.Alisema mara baada ya uchaguzi wa mwaka 2020 waliendeleza tena Serikali ya Umoja wa kitaifa kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar kama ilivyoelekeza, kwa nia ya kuweka jukwaa la kutafuta suluhu ya kudumu ili kujenga maridhiano endelevu na amani ya kudumu Zanzibar aliyoeleza kuwa ni njia pekee ya kujenga uchumi imara, kuondoa umasikini na kujenga nchi kwa ustawi wa wananchi.

Rais Dk. Mwinyi, alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi, Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia kwake kwa vitendo azma ya kuleta maridhiano ya kisiasa nchini ikiwemo kuunda kikosi kazi kilichopitia ripoti ya mkutano wa Baraza la vyama vya siasa na kutoa mapendekezo.

Pia Dk. Mwinyi alimshukuru Dk. Samia kwa uzalendo wake wa kufanya vikao na viongozi wa vyama vya siasa kwa kusikiliza maoni yao na kuyafanyia kazi.
Dk. Mwinyi ambae ni Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi, (CCM) Zanzibar alikishukuru Chama cha ACT Wazalendo, kwa kukubali kukaa pamoja na viongozi wa CCM ili kuendeleza dhamira ya kushirikiana na kuimarisha Umoja wa Kitaifa.

Awali, mwaka 2010 kuliwahi kuundwa Serikali ya Umoja wa kitaifa kufuatia mifarakano ya kisiasa na jamii ikiwemo kuzorota kwa amani mara baada ya kuundwa kwa vyama vingi vya siasa mwaka 1992 ambapo uchaguzi tangu mwaka 1995 na miaka iliyofuata Zanzibar kuliibuka fujo za kisiasa na amani kudorora.Kufuatia marekebisho ya 10 ya katiba ya Zanzibar, Mwaka 2010 kuliundwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa ili kuendeza amani ya kudumu.

Hafla ya uzinduzi wa Kamati ya Maridhiano baina ya Chama cha Mapinduzi na ACT Wazalendo ilihudhuriwa na viongozi wakuu na wajumbe kutoka vyama viwili hivyo, wakiwemo Makamu Mwenyekiti wa Chama cha ACT Wazalendo kwa upande wa Zanzibar ambae pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Othman Masoud Othman, Mjumbe wa Kamati kuu ya Halmashauri kuu ya Chama Cha Mapinduzi ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla, Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, Zanzibar Dk. Muhamed Said Dimwa, Mjumbe wa Halmashauri kuu ya CCM, Dk. Khalid Salum Muhamed ambae pia ni Waziri wa Ujenzi Mawasiliano na Uchukuzi.
Wengine Vuai Ali Vuai ni Mstaafu Naibu Katibu Mkuu CCM Zanzibar pia ni Mjumbe kutoka CCM, Najma Murtaza Giga mjumbe Halmashauri kuu Taifa na Mjumbe wa kamati ya maridhiano kutoka CCM, Salum Hassan Bakari Mjumbe kutoka CCM.

Wengine ni Naibu Katibu Mkuu ACT Wazalendo Zanzibar ambae pia ni Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Nassor Ahmed Mazrui, Omar Said Shaaban Mwanasheria Mkuu wa ACT ambae pia ni Waziri wa Biashara, Mansour Yussuf Himid, Mjumbe Kutoka ACT Wazalendo na Ismail Jussa Ladhu Mjumbe wa Kamati Kuu ACT Wazalendo.