SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema imejikita kuleta mageuzi makubwa kwenye sekta zote za maendeleo pamoja na kuwajengea uwezo watu wake ili kuongeza kasi ya uchumi nchini.Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozungumza na Rais wa Taasisi ya Ufadhili wa masomo nchini Uturuki (YTB) kutoka Wizara ya Utamaduni na Utalii inayoshughulikia Mambo ya Nje, Bw. Abdullah Eren na ujumbe wake waliofika kumtembelea.

Alisema, Serikali imepiga hatua kubwa kuimarisha miundombinu ya kisasa kwa sekta zote za uchumi na jamii ikiwemo kuboresha ujenzi wa barabara, sekta za elimu, afya na uwekezaji.Dk. Mwinyi alisema, Uturuki imekua na ushirikiano wa katibu na Tanzania kupitia ubalozi wake uliopo nchini kwa kuungamkono na kutekeleza miradi mbalimbali ya Serikali ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya barabara, ujenzi wa Uwanja wa Amani na miradi mengine ya jamii, elimu, afya na ujenzi wa nyumba za maakazi kwa wanchi wa Zanzibar kupitia kampuni ya “Orkun” kutoka Uturuki.

Aidha, ameishukuru Serikali ya Uturuki kwa ushirikiano wanaoutoa kwa Serikali za SMT na SMZ hasa kuungamkono juhudi mbalimbali za maendeleo.Rais, Dk. Mwinyi pia, aliipongeza Uturuki kwa kuendelea kuiunga mkono Tanzania ikiwemo Zanzibar, hasa kutoa fursa nyingi za ufadhili wa masomo ya elimu ya juu kwa fani mbalimbali ambapo Watanzania wengi wako nchini Uturuki wakiendelea na mafunzo ya muda mfupi na mrefu.

Alisema, ufadhili ni moja ya msaada mkubwa unaotolewa na Serikali ya Uturuki kwa Tanzania kwenye kukuza ushirikiano mwema uliopo baina ya mataifa mawili hayo.Pia, Dk. Mwinyi aliisifu Uturuki kwa kuwa na wawekezaji wengi Tanzania pamoja na kampuni mbalimbali zinazoendendesha shughuli zao nchini.Alisema kampuni hizo zimekua na ushirikiano mzuri na Seriikali za Tanzania katika kuungamkono na kusaidia kwenye miradi ya maendeleo.

Naye, Bw. Abdullah Eren alimueleza Rais Dk. Mwinyi bado Serikali yao inaendelea kutoa ufadhili wa masomo kwa Tanzania hususan, Zanzibar.Amesema, Serikali ya Uturiki inatarajia kutoa ufadhili mkubwa wa masomo kwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Zanzibar kupitia vyuo vya amali vilivyopo nchini na kumueleza Rais Dk. Mwinyi kwamba tayari wamefanya mazungumzo na Waziri wa Elimu, Lela Muhamed Mussa kujadili suala hilo.

Bw. Aliwapongeza Wazanzibari kwa kuzikimbilia fursa nyingi zinazotolewa na Serikali ya Uturuki na kueleza kuwa asilimia kubwa ya Wazanzibar wako Uturuki kwa masomo na fursa nyengine za maendeleo.Alisema, ujasiri wa Watanzania nchini Uturuki unatokana na ushirikiano na uhisiano mzuri wa Dipolomasia uliopo baina ya pande mbili za ushirikiano.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Balozi wa Uturuki nchini Tanzanzia, Dk. Mehmet Gulluoglu, alimuomba rais Dk. Mwinyi kuangalia uwezekano wa kuipatia fursa Serikali ya Uturi kuanzisha makumbusho ya kidijitali itakayohusisha masuala ya historia na utamaduni ili kuvutia zaidi watalii watakaoingia nchini.Aidha, alieleza fursa hiyo pia itachochoa kasi ya ongezeko la watalii na fursa nyingi za uwekezaji na biashara nchini.


UMOJA WA ULAYA
Wakati huo huo Rais Dk. Mwinyi alizungumza na Naibu Mkurugenzi Mkuu anashughulikia kurugenzi za Jumuiya ya Umoja wa Ulaya, (EU) Martin Seychell, aliefika Ikulu kwa mazungumzo.Katika masungumzo yao pia waligusia masuala mbalimbali ya elimu na sekta nyengine za maendeleo ikiwemo huduma za afya na usalama wa chakula.Rais Dk. Mwinyi, aliishukuru (EU) kupitia Shirika la Kimataifa la “Global Partnership for Education” (GPE) kwa msaada wanaoutoa kwa Tanzania ikiwemo Zanzibar kwenye mfumo mzima wa sekta ya Elimu Zanzibar, kwa ngazi zote kutoka msingi, sekondari hadi vyuo vikuu.

Dk. Mwinyi alieleza licha ya changamoto za Elimu zilizopo, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imejitahidi kuzipatia suluhisho la kudumu kwa msaada wa EU na GPE, ikiwemo kuongeza madarasa mengi yaliyopunguza msongamano wa idadi kubwa ya wanafunzi madarasani kwa wakati mmoja pamoja na kuongeza walimu, kuboresha na kuongeza nyenzo za kufundishia, kuweka miundombinu ya kisasa inayoendana na teknolojia iliopo pamoja na kuimarisha mazingira bora ya skuli za Serikali.

Naye, Bw. Martin Seychell aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa juhudi ilizozichukua kuimarisha sekta ya elimu kwa ngazi zote na kueleza, elimu ndio mustakbali bora wa mageuzi ya uchumi na maendeleo ya dunia.Alisema, kati ya fursa na misaada mingi inayotolewa na EU kupitia shirika la GPE, Zanzibar ni moja kati ya zaidi ya mataifa 30 yanayoendelea duniani, kunufaika na fursa za elimu ikiwemo kutoa mafunzo ya teknolojia kwa walimu wa ngazi za vyuo pamoja na sekondani kwa wasichana.

GPE ni Shirika la Kimataifa kutoka Umoja wa Ulaya (EU) linalotoa ufadhili wa elimu kwa wadau mbalimbali kwa lengo la kuimarisha mifumo bora ya elimu kwa nchi zinazoendelea ili kuongeza kasi ya idadi ya watoto wanaokwenda skuli kusoma. Shirika hilo pia huyaweka pamoja mataifa yanayoendelea, wafadhili, mashirika ya kimataifa, mashirika ya kiraia, mashirika ya walimu, sekta binafsi na Umma.