Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuwa hakuna mbadala wa amani na amewahimiza Waumini wa Dini ya Kiislamu kuendelea kuilinda na kuikuza amani.Ameeleza kuwa Nchi isiyo na amani haiwezi kutekeleza shughuli zozote za maendeleo, na kuwasisitiza Viongozi wa Dini kuendelea kuhubiri amani ili Taifa liweze kusonga mbele kimaendeleo.
Alhaj Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo tarere 12 Disemba 2025 alipojumuika na Waumini wa Dini ya Kiislamu katika Ibada ya Sala ya Ijumaa iliyosaliwa katika Msikiti wa Muhammad (SAW), uliopo Mwanakwerekwe, Mkoa wa Mjini Magharibi. Akizungumzia suala la urafiki ambalo lilikuwa mada kuu katika hotuba ya Ijumaa, Rais Dkt. Mwinyi amesema kuna umuhimu mkubwa kwa vijana kuchagua marafiki wema wenye malezi na maadili mema, huku akiwahimiza wazazi kufuatilia mienendo ya vijana wao ili kuwaepusha na marafiki wasiofaa.
Alhaj Dkt. Mwinyi ameongeza kuwa kwa sasa kuna njia nyingi za kupata marafiki ikiwemo kupitia mitandao ya kijamii, hivyo amewataka vijana kutafakari kwa kina na kuchagua marafiki wema wenye maadili yanayokubalika katika jamii.
