Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewahakikishia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuwa Serikali itaendelea kuweka vivutio na mazingira bora ya uwekezaji kwa lengo la kunufaika na miradi yao.
Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo tarehe 20 Januari 2026, wakati wa uzinduzi wa boti mpya ya Kilimanjaro 9 (Dragon of the Sea) inayomilikiwa na Kampuni ya Azam Marine Ltd, katika hafla iliyofanyika Mtoni Verde, Mkoa wa Mjini Magharibi.
Amesema Serikali inaendelea kuimarisha sekta ya usafirishaji baharini kupitia ujenzi wa miundombinu ya bandari ikiwemo Bandari ya Fumba na bandari nyingine Unguja na Pemba, hatua itakayochochea ukuaji wa uchumi na kuboresha huduma za usafiri baharini.
Rais Dkt. Mwinyi amempongeza Mwanzilishi na Mwenyekiti wa Kampuni ya Azam, Mzee Said Salim Bakhresa, kwa uwekezaji mkubwa unaogusa maisha ya wananchi, akibainisha kuwa kampuni hiyo imewekeza Dola za Marekani Milioni 150 na kutoa ajira 281.
Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Azam, Ndg. Aboubakar Azizi, amesema boti hiyo iliyotengenezwa China ina uwezo wa kubeba abiria 631 na ina mifumo ya kisasa ya kulinda mazingira ya bahari.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa ZIPA, Ndg. Saleh Saad Muhammed, amesema hadi sasa miradi ya uwekezaji yenye thamani ya Dola za Marekani Bilioni 6.8 imesajiliwa, ikitoa ajira 28,000 za moja kwa moja.