Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali inaendelea kutekeleza mikakati na juhudi maalum za kuongeza thamani ya zao la mwani, kwa lengo la kuinua kipato na kuimarisha ustawi wa kiuchumi wa wakulima wa zao hilo. Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 01 Julai 2026, alipokutana na Mratibu Mkaazi wa Umoja wa Mataifa nchini Tanzania, Ndg. Susan Ngongi Namondo, aliyefika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo.

Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali imekipa kilimo cha mwani kipaumbele, kwa kuwa ni miongoni mwa sekta muhimu za kiuchumi zinazotoa ajira na kuwawezesha wananchi wengi kuendesha maisha yao ya kila siku, hususan wanawake ambao wanaunda zaidi ya asilimia 80 ya wakulima wa zao hilo. Ameeleza kuwa, licha ya Zanzibar kuwa kitovu kikuu cha uzalishaji wa mwani nchini na kuchangia kwa kiasi kikubwa kuifanya Tanzania kuwa mzalishaji kinara wa zao hilo barani Afrika, bado sekta hiyo inakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa masoko ya uhakika na kushuka kwa bei.

Amesema hali hiyo imekuwa ikiwafanya wakulima kutonufaika ipasavyo na kazi kubwa wanayoifanya katika uzalishaji wa mwani, hivyo kuathiri juhudi zao za kuongeza kipato na kuboresha maisha yao. Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuondokana na utaratibu wa kuuza mwani kama malighafi, ikiwemo kuanzisha na kuimarisha viwanda vya kusindika mwani ili Zanzibar iweze kuzalisha bidhaa mbalimbali zenye thamani kubwa zaidi.

Amesema hatua hiyo itasaidia kuongeza thamani ya zao la mwani, kupanua masoko, kuimarisha ushindani wa bidhaa za Zanzibar katika soko la kimataifa na kuongeza manufaa yanayopatikana kwa wakulima. Rais Dkt. Mwinyi amesema Zanzibar iko tayari kufanya kazi kwa karibu na Umoja wa Mataifa pamoja na mashirika yake katika kutekeleza programu za kuendeleza kilimo cha mwani, hususan katika maeneo ya mafunzo, teknolojia, upatikanaji wa mitaji na huduma za kifedha.

Amesema ushirikiano huo utasaidia kukifanya kilimo cha mwani kuwa na tija zaidi kwa wakulima na kutoa mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa Zanzibar. Aidha, Rais Dkt. Mwinyi ameuhakikishia Umoja wa Mataifa kuwa Serikali itaendelea kuimarisha ushirikiano wa muda mrefu uliopo, huku akiushukuru Umoja huo kwa mchango na msaada mkubwa unaotolewa kupitia mashirika yake, yakiwemo UNESCO, UNDP na UNICEF.

Amesema mashirika hayo yameendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika sekta mbalimbali, ikiwemo afya, elimu, kilimo, maendeleo ya jamii na ujenzi wa uwezo wa rasilimali watu.

Naye Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini Tanzania, Ndg. Susan Ngongi Namondo, amesema Umoja wa Mataifa unaendelea kuchukua hatua za kuimarisha kilimo cha mwani kama sehemu muhimu ya maendeleo ya sekta ya Uchumi wa Buluu. Amesema Umoja wa Mataifa utaendelea kushirikiana na Zanzibar kupitia programu mbalimbali zinazolenga kuendeleza zao la mwani, kuongeza thamani yake na kuwawezesha wakulima kunufaika zaidi kiuchumi.

Ndg. Susan amefahamisha kuwa, katika juhudi za kuwavutia wadau na wawekezaji kuwekeza katika sekta ya mwani, Umoja wa Mataifa unakusudia kuandaa filamu maalum ya kuitangaza Zanzibar, kilimo cha mwani na fursa zake katika jumuiya ya kimataifa.

Wakati huohuo, Rais Dkt. Mwinyi amekutana na Balozi wa Palestina nchini Tanzania, Mhe. Salam Abu Sharar, aliyefika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo maalum. Mazungumzo hayo yamejikita katika kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia, kiuchumi na kijamii baina ya Zanzibar na Palestina.

Rais Dkt. Mwinyi amewakaribisha wawekezaji kutoka Palestina kuja kuwekeza Zanzibar katika sekta mbalimbali, ikiwemo nishati, mafuta na gesi, utalii na Uchumi wa Buluu. Amesema Zanzibar itaendelea kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji na kuimarisha ushirikiano na washirika wa kimataifa katika utekelezaji wa miradi yenye manufaa …