RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein ameungana pamoja katika futari maalum aliyoiandaa yeye na familia yake kwa ajili ya wananchi mbali mbali wakiwemo majirani zao huko katika makaazi yake Kibele, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja.
Hafla hiyo ya futari ilifanyika katika viwanja vya nyumbani kwake Kibele na kuhudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, viongozi wa dini, Serikali, vyama vya siasa, wananchi wa kijiji hicho pamoja na vijiji vya jirani.
Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein nae aliungana na viongozi wa kike wa Kitaifa, wanafamilia pamoja na wananchi mbali mbali wakiwemo majirani zake katika hafla hiyo ya futari maalum waliyoiandaa.
Akitoa neno la shukurani kwa niaba ya Alhaj Dk. Shein pamoja na familia yake, mwanafamilia Mohamed Ali Shein aliwashukuru waalikwa wote waliofika katika hafla hiyo na kufutari.
Katika maelezo yake, Mohamed Shein alieleza kuwa familia hiyo imefarajika sana kwa waalikwa hao kukubali mwaliko huo na kufika kwa wingi katika futari hiyo maalum waliyoiandaa.
Aidha, Alhaj Dk. Shein aliwaombea dua kwa Mwenyezi Mungu wananchi wote na viongozi waliohudhuria katika futari hiyo kuendelea kupata neema na baraka za Allah hasa katika kipindi hichi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
Alhaj Dk. Shein na familia yake wamekuwa na utamaduni wa kila mwaka katika mwezi Mtukufu wa Ramadhani kuandaa futari maalum na kuwaalika wanakijiji, majirani pamoja na waalikwa wengine wakiwemo viongozi wa Serikali, dini na vyama vya siasa, futari ambayo hufanyika huko katika makaazi yake Kibele, Mkoa wa Kusini Unguja.