RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuridhishwa na utekelezaji wa shughuli mbalimbali za chama na serikali zilizotekelezwa katika Wilaya ya Magharibi ‘B’.
Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo katika Majumuisho ya ziara yake ya Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini Magharibi yaliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Zanzibar Beach Resort Mazizini, mjini Zanzibar ambapo viongozi mbali mbali walihudhuria akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Mama Mwanamwema Shein na viongozi wengine.
Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alipongeza juhudi zilizochukuliwa na uongozi wa Wilaya hiyo katika kuendeleza na kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwa ni pamoja na mashirikiano mazuri yaliopo kati ya uongozi wa Wilaya na uongozi wa Chama.
Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inazozichukua katika kuhakikisha inawapelekea huduma bora wananchi wake wote bila ya kujali rangi, dini, kabila wala itikadi ya kisiasa.
Alipongeza kwa taarifa nzuri ya Wilaya iliyotolewa katika majumuisho hayo ambayo imeonesha wazi kuwa kazi kubwa imefanywa tena kwa mafanikio mazuri.
Dk. Shein alieleza furaha yake iliyompelekea kuridhika na ziara hiyo kwa kuona miradi muhimu ya maendeleo ambayo ameiwekea mawe ya msingi kikiwemo kituo cha afya Magirisi pamoja na Skuli ya Msingi ya Kwarara katika Wilaya hiyo.
Aidha, Dk. Shein alisisitiza haja kwa vituo vya afya vinavyohudumia watu ni vyema vikaandaliwa vizuri katika kutoa huduma na kuitaka Wizara ya Afya kujipanga vyema kabla ya kuanza kutoa huduma katika kituo hicho pale kitakapokuwa tayari.
Alieleza kuwa kuwepo kwa amani na utulivu hapa Zanzibar kumeweza kuwavutia wageni kutoka nchi mbali mbali duniani kuja kuitembelea Zanzibar na kusisitiza haja ya kulindwa na kuenziwa ili Zanzibar izidi kupata mafanikio ikiwemo kuongezeka kwa watalii.
Alisema kuwa ili Zanzibar iweze kufika katika uchumi wa Kati nguvu kubwa zinahitajika katika kuimarisha sekta ya elimu na kusisitiza kuwa iwapo Zanzibar ikitaka kuimarisha sekta ya elimu ni lazima elimu ya msingi iimarishwe.
Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuupongeza uongozi wa Wilaya, uongozi wa Wizara ya Elimu kwa mashirikiano makubwa yaliopo ambayo yamepelekea kujengwa kwa Skuli mpya ya Msingi ya Kwarara.
Nae Waziri wa Nchi Afisi ya Rais Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Haji Omar Kheir alieleza kuwa mbali ya Wakuu wa Wilaya kusubiri ziara za viongozi pia, wanajukumu la kuzishughulikia changamoto za wananchi.
Mkuu wa Wilaya ya Magharibi ‘B‘ Kapteni Silima Haji Haji akitoa taarifa ya Wilaya hiyo alieleza katika kufanikisha zoezi la ukusanyaji wa mapato Baraza la Manispaa lilipanga mikakati mbali mbali na njia za utekelezaji wake ili liweze kufikia malengo ya ukusanyaji mapato ya TZS Bilioni 2 kwa mwaka 2018/2019 sawa na ongezeko la asilimia 35 ya makisio ya mwaka 2017/2018 ambayo yalikuwa TZS bilioni 1.3.
Aliongeza kuwa njia za ukusanyaji wa mapato zimeimarishwa ikiwemo kuanzisha mfumo wa kukusanyia mapato wa kielektroniki ambapo jumla ya ‘Point of Sale’ (POS) 19 zimenunuliwa.
Kwa upande wa sekta ya elimu alisema kuwa mafanikio makubwa yanaendelea kupatikana yakiwemo ya uandikishaji wa wanafunzi wapya ambapo kwa upande wa elimu ya awali uandikishaji umepanda kutoka wanafunzi 3,009 mwaka 2018 hadi wanafunzi 3,225 mwaka 2019 huku akieleza mikakati iliyowekwa ya elimu ya Sekondarinkatika Wilaya hiyo.
Aidha, alieleza juhudi zinazochukuliwa katika kupambana na vitendo vya udhalilishaji wa wanawake na watoto zinavyoendelea ambapo muitiko wa kuripoti matukio hayo unaonekana kuongezeka ingawa changamoto iliyokuwepo ni pamoja na baadhi ya wananchi kukataa kutoa ushahidi pindi wanapohitajika kufanya hivyo.
Alisema kuwa Serikali kupitia Mamlaka ya Maji imeweza kwa kiwango kikubwa kuimarisha miundombinu ya maji ndani ya Wilaya hiyo hivi sasa Shehia zimeunganishwa na zinapata maji safi na salama kutokana katika visima 22 vya Serikali kutegemea utaratibu uliopangwa.
Katika juhudi za kuwapatia huduma ya maji safi na salama katika Wilaya hiyo, Mkuu huyo wa Wilaya alieleza kuwa Serikali kwa kushirikiana na Washirika wa Maendeleo inatarajia kuanza kwa mradi wa maji utakaogharimu Dola za Marekani Milioni 92.8 ambao utapunguza tatizo la maji safi na salama kwa wananchi wa Wilaya hiyo.
Aliongeza kuwa Mradi huo utahusisha uchimbaji wa visima, ujenzi wa matenki na ulazaji wa mabomba katika maeneo mbali mbali likiwemo eneo la Kwarara Kidutani.
Akitoa neno la shukurani Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Ayoub Mohammed Mahmoud alisisitiza haja ya kufanya kazi kwa mashirikiano na kueleza kuwa watayafanyia kazi yale waliyoelekezwa na Rais Dk. Shein katika majumuisho hayo.
Alisema kuwa Rais Dk. Shein ametoa elimu klubwa katika ziara yake kwenye Wilaya zote tatu na kueleza kufarajika kwa namna Dk. Shein kumaliza ziara yake katika Mkoa huo akiwa na furaha tele kutokana na kazi kubwa iliyofanywa na kuahidi kuwa changamoto zilizoelezwa jitihada zitafanyika ili kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi.
Rais Dk. Shein anatarajia kuendelea na ziara yake katika Mkoa wa Kaskazini itakayoanzia katika Wilaya ya Kaskazini A Unguja siku ya Jumaapili ya tarehe 17 Februari mwaka huu 2019.