RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mheshimiwa Dk. Ali Mohamed Shein, amewaahidi wananchi wa Kitogani kuwa uwanja wao utatengenezwa kwa kiwango cha Kimataifa kitakachoshirikisha michezo ya aina mbali mbali.

 

Dk. Shein aliwaeleza wananchi hao wa kijiji cha Kitogani kuwa kijiji chao kitakuwa eneo la michezo kwani watafika watu kutoka ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kuutumia uwanja wao mpya unaoendelea kujengwa ambao tayari kwa awamu ya kwanza umekamilika.

Hivyo, amewataka wakaazi wa Kitogani kujiandaa kuwapokea wageni wakiwemo wanamichezo huku akieleza jinsi Serikali ilovyojiandaa kukijenga kiwanja hicho kuwa cha kisasa na kuweza kuchezwa michezo kadhaa mbali na mpira wa miguu.

Alieleza kuwa miongoni mwa juhudi zitakazochukuliwa na Serikali anayoiongoza ni pamoja na kuuwekea mpira wa kukimbilia, majani bandia kama yaliopandwa halitodumu, taa na kujengwa majukwaa ya kukaa pamoja na mambo mengine yote muhimu yanayopaswa kuwepo kiwanjani hapo.

Dk. Shein alisema kuwa ujenzi wa kiwanja hicho ni utekelezaji wa ahadi aliyowaahidi wananchi wa Kitogani baada ya wazee kutoa ombi lao la kujengewa uwanja vijana wao na kusisitiza kuwa juhudi atazifanya katika kuhakikisha kiwanja kinakamilika katika wakati wake wa uongozi.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa nia ya Chama chake cha CCM ni kuimarisha michezo.

Aidha, Dk. Shein alieleza kuvutiwa kwake na mashindano ya riadha ya Wilaya yaliyofanywa mnamo mwaka 2014 na mshindi alitoka Wilaya ya Kati katika kijiji cha Ndijani na kuyapongeza mashindano hayo.


Dk. Shein alisisitiza kuwa michezo ni afya, ajira, hujenga umaarufu sambamba na kuzidisha uhusiano na ushirikiano kwa wanamichezo na ndio maana akaanzisha siku ya mazoezi kila inapofika Januari mosi ya kila mwaka ambapo imeweza kuwahamasisha wananchi wengi ambapo hivi sasa wamekuwa wakifanya mazoezi.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alitoa pongezi kwa wananchi wa Kitoganai na hasa wale waliobomoa nyumba zao tano za makaazi na kupitisha ujenzi wa kiwanja hicho paoja na shukurani kwa Mbunge wa Jimbo la Tunguu kwa mchango wake katika ujenzi huo.

Mapema Katibu Mkuu, Wizara ya Habari,Utamaduni, Utalii na Michezo Omar Hassan alieleza kuwa kwa awamu ya kwanza uwanja huo utagharimu TZS milioni 146 huku akieleza kuwa kiwanja hicho ni miongoni mwa viwanja 5 vinavyojengwa Unguja na Pemba.

Alieleza kuwa awamu ya Pili ya ujenzi wa uwanja huo itakuwa ni pamoja na ujenzi wa ukuta wa uzio na kusisitiza kuwa ujenzi huo ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 ya kutaka kujengwa viwanja 5 katika Mikoa ya Zanzibar. 

Nae Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Zanzibar Sharifa Khamis alieleza kuwa ujenzi wa kiwanja hicho unajengwa kwa kiwango cha Kimataifa na kusisitiza kuwa kwa vile awamu ya kwanza ya ujenzi wa kiwanjahicho umekuwa tayari hivi sasa wanaelekea Pemba huko Micheweni kujenga kiwanja kama hicho na baadae kuendelea na viwanja vyenginevyo Unguja na Pemba vikiwemo Langoni na kangani.

Nao wananchi katika kijiji cha Kitogani walitoa shukurani zao kwa Rais Dk.
Shein kwa kuwajengea uwanja wao huo kwani jitihada zao wenyewe zilichukua muda wa miaka 15 lakini hawakufanikiwa.

Wananachi hao walieleza kuwa kasi ya ujenzi wa kiwanja hicho ilianza kuonekana pale tu alipoanza kumkabidhi kazi Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Sharifa Khamis na kusimamia ujenzi huo na kuifanya kazihiyo vyema kwa mashirikiano na watalamu mbali mbali.

Aidha, wananchi hao walieleza azma yao ya kutekeleza kwa vitendo mpango wa Serikali wa Utalii kwa wote kwa kutumia rasilimali zilizopo. Wananchi hao pia, walitoa pongezi kwa Dk. Shein kwa namna anavyosimamia utekelezaji wa Ilani ya CCM na kuwapelekea wananchi maendeleo ya kupigiwa mfano Unguja na Pemba.