Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewasisitiza Waumini wa Dini ya Kiislamu kuitumia misikiti kama vituo muhimu vya kujadili na kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii, sambamba na kutoa ufumbuzi unaofaa kwa maendeleo ya jamii.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo tarehe 23 Januari 2026, baada ya kujumuika na Waumini wa Dini ya Kiislamu katika Sala ya Ijumaa iliyofanyika katika Msikiti wa Ijumaa wa Mfereji wa Wima, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Amesema kuwa changamoto zilizopo katika jamii ni nyingi, hivyo ni wajibu wa Waumini kushirikiana kupitia misikiti kwa kuhamasisha michango itakayosaidia familia na jamii duni zisizojiweza.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amepongeza uongozi wa Msikiti wa Mfereji wa Wima kwa kuanzisha na kuendesha utaratibu wa ukusanyaji wa michango kwa ajili ya kusaidia wahitaji.

Katika kuunga mkono jitihada hizo, Rais Dkt. Mwinyi ameahidi kuchangia Shilingi Milioni 34 kwa ajili ya kuimarisha mfuko wa msikiti huo, huku akiwahimiza Waumini wa Dini ya Kiislamu kuendelea kutoa michango yao kwa moyo wa kujitolea ili kuwasaidia wenzao wenye uhitaji.