MKE wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Mama Mariam Mwinyi ameiasa jamii kujitahidi kukithirisha ibada ndani ya mwezi huu Mtukufu wa Ramadhan na kutoa sadaka kwa wingi hasa kuwafikia watu wenye mahitaji maalumu wakiwemo wazee, watoto yatima, wenyeulemavu na masikini ili kupata radhi za Mwenyezi Mungu (S.W).

Mama Mariam Mwinyi ambae pia ni Msarifu na Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Zanzibar Maisha Bora Foundation (ZMBF), aliyasema hayo kwa nyakati tofauti kwenye ziara yake aliyowakilishwa na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Anna Athanas Paul alipowatembelea wazee wa Welezo na Sebleni, watoto yatima waliopo Kijiji cha SOS na Mazizini, pamoja na kituo cha kulelea watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu, kilichopo Fuoni Mambosasa (ZASO), Mkoa wa Mjini Magharibi ambako aliwasalimia, kuwafariji na kuwapa zawadi ya futari.

Alisema, ibada ya sadaka sio lazima kutolewa zaidi kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani, bali hata siku za kawaida kwani zinaogeza upendo na kuigusa jamii yenye uhitaji.“Kama kawaida desturi yetu mwezi wa Ramadhan huwa tunatembeleana, kujuliana hali, sio desturi pekee lakini pia ni maagizo kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, anatutaka waja wake kutoa sadaka kwa wingi na kufanya zaidi mambo mazuri ya kumridhisha Yeye kama kuwakumbuka wazee, wajane, watu wasiojiweza na masikini kuwapa sadaka ili nao watekeleza vizuri ibada hii ya mwezi mtukufu wa Ramandani” Alisema Mama Mariam.

Mama Mariam alitumia fursa hiyo kuwafikishia salamu za Rais wa Zanzibar na kuwaeleza kwamba yupo pamoja nao wakati wote wa mfungo wa mwezi huu mtukufu wa Ramadhani.Alisema, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuyaenzi matunda ya Mapinduzi bado inaendelea kuwajali na kuwaenzi wazee kwenye nyumba maalumu pamoja na watotoyatima ambao Serikali inawaangalia kwa jicho la karibu.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Mkurugenzi wa Idara ya Ustawi wa Jamii na Wazee, Hassan Ibrahim Suleiman na Mkurugenzi wa kituo cha kulelea watoto yatima SOS, Asha Salum Ali waliishukuru ziara ya Mama Mariam kwenye taasisi hizo na kueleza msaada alioutoa kwa wazee na watoto hao umewafikiwa wakati sahihi.

Walieleza, licha ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutoa huduma kama hizo kila mwezi katika jitihada zake za kuwaenzi na kuwatunza watu wenye mahitaji maalum, pia msaada huo alioutoa Mama Mariam Mwinyi utaongeza tija na kuwasaidi wakati huu wenye uhitaji.Pamoja na mambo mengine Wakurugenzi hao pia walimuombea dua na mtakia kheir Mama Mariam Mwinyi kwa jitihada zake anazozitoa kwa makudi maalum.

Pia, wakurugenzi hao kwa niaba ya walenzi na wafanyakazi wa taasisi hizo walimuombea dua na makazi mema peponi, Mwanzilishi wa kituo cha kulelea watoto yatima cha SOS, Marehemu Mzee Ali Hassan Mwinyi, Rais Mstaafu wa Zanzibar na Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, aliefariki hivi karibuni na kueleza msaada huo umekuja kama sadaka kwao.
Miongoni mwa msaada waliopatiwa wazee na watoto hao ni pamoja na tende, vyakula vikiwemo mchele, unga wa ngano, sembe, mafuta ya kupikia, sukari pamoja na vyakula vya nafaka.