Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewasisitiza viongozi wakuu katika taasisi za umma kuzingatia upendo, uadilifu na haki katika kuwasimamia wanaowaongoza pamoja na utekelezaji wa majukumu yao.Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 8 Machi 2026, katika Kongamano la Tatu la Kiimani kwa Viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar lililoandaliwa na Afisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar na kufanyika katika Ukumbi wa Sheikh Idris Abdul Wakil, Kikwajuni, Mkoa wa Mjini Magharibi.
Ameeleza kuwa kongamano hilo ni msingi muhimu wa kukumbushana umuhimu wa kuzingatia maadili katika utumishi wa umma na ni jukwaa muhimu la kujifunza uwiano wa kazi kwa misingi ya kiimani, jambo litakaloleta mafanikio na ufanisi katika utendaji wa taasisi za Serikali. Aidha, Rais Dkt. Mwinyi ametoa wito kwa viongozi wa umma kulitumia kongamano hilo kuwa dira ya kusimamia majukumu yao kwa wema, uadilifu, haki na busara, huku wakizingatia kuwa uongozi ni dhamana.
Akihitimisha hotuba yake, Rais Dkt. Mwinyi amewataka viongozi kuyapokea maelekezo yaliyotolewa na Masheikh katika mada zilizowasilishwa kwenye kongamano hilo na kuyatumia kama nyenzo ya kuleta mabadiliko katika utekelezaji wa majukumu yao huku wakitanguliza imani.
Rais Dkt. Mwinyi ameipongeza Afisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar pamoja na Wizara ya Nchi, Afisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora kwa kuandaa kwa mafanikio kongamano hilo kwa miaka mitatu mfululizo.
Kongamano hilo limehudhuriwa na viongozi wa ngazi mbalimbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama, viongozi wa dini pamoja na watumishi wa SMZ.