RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi ameihimiza jamii kujikita kwenye malezi yenye maadili ya kiislamu kwa watoto na vijana ili wawe na tabia njema zitakazomridhisha Mwenyezi Mungu (S.W).Al - hajj Dk. Mwinyi alitoa nasaha hizo wakati wa ufunguzi wa msikiti wa masjid Al - Jumaa, uliopo Dunga Kiembeni, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja.
Alisema jamii imegubikwa na wingu la matatizo yanayosababishwa na mporomoko wa maadili, kujaa madhila ya udhalilishaji, kuongezeka kwa matumizi ya dawa za kulevya, wizi wa mazao ya kilimo na mifugo kulikosababishwa na kukosa malezi bora yenye hofu ya uchamungu ukosefu wa maadili.“Vijana wetu wafundishwe dini yao vizuri, wafundishwe kitabu cha Mwenyezi Mungu, wafundishwe tabia njema, tutapunguza matatizo yanayotokea ukubwani” Aliasa Dk. Mwinyi.
Al - hajj Dk. Mwinyi pia alizinasihi jamii kutumia nyumba za ibada kuwafundisha vijana mustakbali mwema wa ustawi wa maisha yao kupitia madrsa na nyumba za ibada ikiwemo misikiti, aliongeza malezi hayo yanaanzia kwenye nyumba za ibada ili kuondosha matatizo yanayoisumbua jamii.Akieleza neema za mwezi mtukufu wa Ramadhani, Al - hajj Dk. Hussein Mwinyi aliwasihi jamii kukithirisha ibada na kujitahidi kwenye kuongeza ibada ya sala za taraweikh aliyoieleza kwamba inakuja mara moja tu kwa mwaka pamoja na kuwanasihi waumini wa msikiti huo, kuendeleza ibada za sala za sunnah.
Hata hivyo, Al - hajj Mwinyi aliahidi kuujengea uzio msikiti huo ili uiendaene na hadhi yake na uendelee kudumu na kuwa imara.Hakika hatua nyengine Al - hajj Dk. Mwinyi aliwataka waumini wa msikiti huo kuendelea kuutunza na kuuenzi ili udumu kwaajili ya vizazi vya sasa na baadae.Akizungumza kwenye ibada hiyo ya sala ya Ijumaa, Katibu Mtendaji kutoka Ofisi ya Mufti Zanzibar, Khalid Ali Mfaume aliwasihi waumini wa din
i ya kiislamu kuutumia vyema Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa kujitathmini na kujipima mema na mabaya yao mbele ya Mwenyezi Mungu kwa kuongeza bidii ya kufanya ibada hasa kwa siku chache zilizobakia kabla ya kumalizika kwa ibada ya mfungo wa mwezi huo.“Huu ndio mwezi wa kikuthirisha kheri na kufanya mazuri zaidi yatakayompendezesha Mwenyezi Mungu, ili kupata msahama wake na sio kupoteza muda na kuanzisha michezo isiyo na tija kwenye jamii” Alishauri Katibu huyo.
Mapema, akisoma risala ya ufunguzi wa msikiti huo Ustadhi Abdalla Makame Makame, alisema ujenzi wa msikiti ulichukua miezi minne tokea kunza hadi kukamilika kwake.Alieleza ulianza kujengwa Novemba 11 mwaka 2022 na ulikamilika tarehe 13/03/2013 ambao unatarajiwa kuchukua hadi waumini 612. Pia alieleza ujenzi wa msikiti huo ulikuja kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ikiwemo ufinyu wa nafasi kwa msikiti wa awali uliosababishwa na kuongezeka kwa waumini wengi kijijini hapo baadhi yao wakiwa wahamiaji katika eneo hilo.
Ust. Makame aliongeza sababu nyengine ya kujengwa kwa msikiti huo ni kupisha utanuzi wa ujenzi wa barabara inayotarajiwa kutoka Dunga Mitini kuelekea Chwaka.
Ujenzi wa msikiti wa masjid Al – Jumaa uligharimu shilingi milioni 178.148 ambao ulifadhiliwa na shekh Said Saleh.